Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 7 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 88 2020-02-05

Name

Goodluck Asaph Mlinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulanga

Primary Question

MHE. GOODLUCK A. MLINGA aliuliza:-

Nchi yetu imebarikiwa kuwa na Hifadhi nyingi zenye wanyama wengi wa kuvutia lakini mapato yatokanayo na utalii ni kidogo: Je, Serikali ina mikakati gani ya kuongeza mapato ya utalii?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Goodluck Asaph Mlinga, Mbunge wa Ulanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Utalii imeendelea kukua mwaka hadi mwaka. Mathalan idadi ya watalii imeongezeka kutoka 1,137,182 mwaka 2015 hadi kufikia watalii 1,505,702 mwaka 2018. Katika kipindi cha mwaka 2018 pekee Sekta hii imechangia katika uchumi wa nchi Dola za Marekani bilioni 2.4, sawa na takriban trilioni 5.4. Sekta hii imechangia kwa wastani wa asilimia 17 ya Pato la Taifa na asilimia 25 ya fedha za kigeni. Aidha, inatoa ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja milioni 1.6. Hata hivyo, kiwango cha mchango wa sekta hii bado ni kidogo ukilinganisha na rasilimali tulizonazo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo, Wizara yangu imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchini na mchango utokanao na sekta hii. Mikakati hiyo ni pamoja na kupanua wigo wa mazao ya utalii kijiografia kupitia Mradi wa REGROW ambapo Serikali inaendelea kufungua utalii katika Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini kwa kuimarisha miundombinu ili kuboresha shughuli za utalii hususani katika hifadhi za Taifa za Ruaha, Udzungwa, Mikumi na Nyerere. Aidha, Serikali imeanzisha Hifadhi mpya za Taifa sita ambazo ni pamoja na Burigi-Chato, Ibanda-Kyerwa, Rumanyika-Karagwe, Mto Ugalla, Nyerere na Kigosi. Lengo la Serikali ni kufungua na kutumia fursa za utalii nchini katika mikoa yote.

Mheshimiwa Spika, kadhalika Serikali imekusudia kuongeza mazao ya utalii. Hivi sasa, hapa nchini tumejikita zaidi katika kuziendeleza hifadhi za Taifa. Tunataka kuhakikisha kw amba mazao mengine ya utalii kama utalii wa kuvinjari kwa meli, utalii wa kupunga upepo fukwe na utalii wa mikutano ukiongezeka.

Mheshimiwa Spika, sanjari na juhudi hizo, Mwezi Septemba, 2019 Wizara yangu kwa kushirikiana na Nyanda za Juu Kusini iliandaa kwa kushirikiana na Sekta Binafsi maonesho makubwa ya utalii Jukwaa la Uwekezaji yajulikanayo kama Karibu Utalii Kusini ambapo zaidi ya washiriki mia tano kutoka ndani na nje ya nchi walishiriki. Vilevile, Mwezi Oktoba, 2019 Wizara iliandaa Onesho la Kimataifa la Utalii la Swahili International Tourism Expo lililohusisha wafanyabiashara wakubwa wa utalii takribani 400 na Mawakala wa Kimataifa 200 kutoka ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa sasa Wizara kwa kushirikiana na Mikoa ya Kanda ya Ziwa, Kigoma na Tabora imeanza maandalizi ya maonesho makubwa ya Kimataifa ya jukwaa la utalii na uwekezaji yanayojulikanayo kama Great Lakes International Tourism Expo ambayo yatafanyika Mwezi Juni, 2020. Imani yangu kuwa mikakati hii itasaidia kutangaza vivutio vya utalii, vya uwekezaji na kuongeza watalii nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mikakati hiyo, Wizara imeendelea kuimarisha shughuli za utangazaji wa vivutio vya utalii wa kimataifa, ikiwa ni pamoja na kufungua masoko mapya nchini China, India, Urusi na Israeli. Aidha, katika kudhibiti upotevu wa mapato ya Serikali, Wizara imekamilisha ujenzi wa mfumo funganishi wa kieletroniki kwa ajili ya kusajili na kutoa leseni, na kukusanya takwimu sahihi.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Awamu ya Tano, katika kuboresha miundombinu nchini ikiwemo viwanja vya ndege, ujenzi wa reli, upanuzi wa bandari, kuimarika kwa Shirika la Ndege ambalo limeanza kuhudumia watalii wa ndani na nje ya nchi. Juhudi hizi zitasaidia sana kukuza Sekta ya Utalii nchini. (Makofi)