Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 16 2019-09-04

Name

Dr. Joseph Kizito Mhagama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Madaba

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA aliuliza:-

Moja kati ya maombi yaliyowasilishwa kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati wa ziara yake Mkoani Ruvuma, katika Wilaya ya Songea ni zahanati za Mbangamawe na Magingo zilizoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Madaba zitakapokamilika zipandishwe hadhi kuwa Vituo vya Afya kutokana na ukubwa wake na mahitaji kwa Wananchi:-

Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza jukumu hilo muhimu?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama Mbunge wa Madaba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa akiwa ziarani Mkoani Ruvuma tarehe 05 Januari, 2017 katika Halmashauri ya Madaba alipokea maombi kutoka kwa wananchi ya kuiomba Serikali kuzipandisha hadhi Zahanati za Magingo na Mbangamawe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini iliyofanyika imebaini kuwa ujenzi wa Zahanati zote mbili umefikia asilimia 45 kila zahanati ina jengo moja kubwa lenye vyumba 21 kwa kufuata ramani zilizotolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kabla ya mwaka 2010 kwa kuzingatia mpango wa MMAM. Vyumba 5 kati ya 21 kwa kila zahanati vimekamilika. Tathmini inaonyesha kuwa ili kukamilisha ujenzi kiasi cha shilingi milioni120 kinahitajika kwa zahanati ya Mbangamawe na milioni 100 kwa zahanati ya Magingo. Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha ili kukamilisha na kufuata taratibu zote zinazotakiwa ili kuzipandisha hadhi zahanati hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuendelea kuboresha huduma za afya Madaba katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imepatia Halmashauri ya Madaba kiasi cha shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati, ujenzi na upanuzi wa vituo vya afya vya Madaba, Mtyangimbole. Vilevile katika bajeti ya mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Madaba. Serikali inaendelea na jitihada za kujenga, kukarabati, kupanua na kuboresha miundombinu ya afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.