Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 5 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 65 2020-02-03

Name

Taska Restituta Mbogo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-

Watanzania wengi wanaoishi nje ya nchi wamejikuta ni raia wa nchi wanazoishi kwa sababu mbalimbali ikiwemo kazi lakini si kwamba hawaipendi Tanzania:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwatambua Watanzania waliochukua uraia wa nchi nyingine ili waweze kukuza uchumi wa nchi na kusaidia ndugu zao?

Name

Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kusimamia masuala yanayohusu Watanzania wanaoishi nje ya nchi (diaspora) pasipo kubagua wale waliochukua uraia wa nchi nyingine kwa lengo la kuhakikisha kuwa mahitaji yao ya kikonseli yanashughulikiwa na pia kuongeza ushiriki wao katika kuchangia maendeleo ya nchi na ndugu zao.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeweka mikakati mbalimbali ya kuwatambua diaspora katika kukuza uchumi. Mikakati yao ni pamoja na kuhimiza diaspora kujisajili kwenye Balozi zetu na maeneo ya uwakilishi; kuratibu makongamano ya diaspora ndani na nje ya nchi; kuratibu mikutano ya diaspora na viongozi wa Serikali wanapofanya ziara za kikazi nje ya nchi; kuhamasisha diaspora kuunda na kusajili jumuiya zao na kuwahimiza kuwa washawishi wazuri wa uwekezaji kutoka mataifa mengine kuja kuwekeza nchini.

Mheshimiwa Spika, idadi ya diaspora wa Kitanzania nje ya nchi inakadiriwa kuwa ni zaidi ya milioni moja, ambapo idadi ya diaspora waliojisajili kwa hiari kwenye Balozi zetu na maeneo ya uwakilishi ni takribani laki moja. Aidha, diaspora hao wamekuwa wakimiliki akaunti kwenye taasisi mbalimbali za kifedha kama vile Benki za Azania, CRDB, NMB, Stanbic na pia kuwa wanachama wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya NSSF na PSSSF, ikiwa ni pamoja na kumiliki nyumba 166 zilizouzwa na Shirika la Nyumba la Taifa zenye thamani ya shilingi bilioni 5.5 hadi kufikia Februari, 2019. Pia diaspora wameleta mafanikio makubwa kwa ndugu zao na taifa kwa ujumla kwa kuchangia sekta mbalimbali kama vile afya ambapo tumekuwa tukipokea wataalam wa afya na magonjwa yenye kuambukiza na yale yasiyoambukiza kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, tunao mfano mzuri katika sekta ya afya ambapo Novemba, 2019 tulipokea msaada wa sanamu ya vitendo (simulative manikin) kutoka kwa Jumuiya ya Watanzania Wanaoishi Uingereza yenye thamani ya shilingi milioni 100; vitabu vya afya vyenye thamani ya shilingi milioni 30 vilivyogawiwa katika Maktaba Kuu ya Shirika la Elimu Kibaha, Taasisi ya Jakaya Kikwete, Hospitali ya Namanyere iliyopo Sumbawanga, Mkoa wa Rukwa, Mbeya pamoja na Pemba.