Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 3 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 30 2020-01-30

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Katika miaka ya hivi karibuni nchi yetu imekuwa na majina mengi katika Idara ya Ukaguzi toka Ofisi ya CAG kama vile Hati safi, Hati inayoridhisha na Hati chafu:-

(a) Je, Shirika au Halmashauri kupata hati safi ni ishara kwamba Shirika au Halmashauri husika halina ubadhirifu wa mali ya Umma kwa kuwa kuna kila dalili kuwa kutolewa kwa hati safi ni dalili ya wazi ya kuficha ubadhirifu katika baadhi ya Mashirika na Taasisi za Umma?

(b) Je, lini Serikali itafuta utaratibu huo ambao umekuwa kinga ya ubadhirifu wa mali ya Umma?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Boniphace Getere, Mbunge wa Bunda, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Ukaguzi wa Umma ya Mwaka 2008 inampa mamlaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kufanya kaguzi mbalimbali ambazo ni Ukaguzi wa Hesabu (Financial Audits), Ukaguzi wa Kiuchunguzi (Forensic Audits), Ukaguzi wa Ufanisi (Performance Audits) na Ukaguzi Maalum (Special Audits). Lengo Kuu la Ukaguzi wa Hesabu (Financial Audits) ni kutoa maoni kama Hesabu zinazokaguliwa zinaonyesha hali halisi ya mapato na matumizi ya Serikali kwa kuzingatia Viwango vya Kimataifa vya Uandaaji wa Taarifa za Fedha. Maoni haya hutolewa kwa njia ya hati za ukaguzi ambazo zimegawanyika katika makundi manne ambayo ni hati inayoridhisha; hati yenye shaka hati isiyoridhisha na hati mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hati inayoridhisha hutolewa wakati taarifa za fedha zilizowasilishwa na kukaguliwa zinapokuwa zimezingatia Viwango vya Kimataifa vya Uandaaji wa Hesabu katika Sekta ya Umma na Sheria na Kanuni za Fedha za Umma. Hati hii huonesha taarifa za fedha zinatoa taswira ya kweli na hali halisi ya mapato, matumizi, mali na madeni ya taasisi husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya kuwa ‘hati inayoridhisha’ inatoa tafsiri ya kutokuwepo kwa kila aina ya ubadhirifu siyo sahihi kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, maoni ya ukaguzi yanatolewa kwa malengo maalum ya kuwafahamisha watumiaji wa taarifa za fedha kama taarifa hizo zinaonyesha ukweli na hali halisi ya hesabu za mizania (financial positions) kwa tarehe husika, taarifa za mapato na matumizi (financial performance) pamoja na taarifa ya mtiririko wa fedha (cash flows) kwa kipindi kilichokaguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, dhana ya ukaguzi wa hesabu inajikita katika masuala ambayo wakaguzi wanaamini kuwa ni mazito na yana athari kubwa kwenye taarifa za fedha za taasisi husika. Hii ina maana kuwa, mambo ambayo hayana athari kwenye taarifa za fedha yanashughulikwa na mifumo ya udhibiti wa ndani ya taasisi husika.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majibu haya ya sehemu (a), napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, utaratibu huu ndiyo unaotumika dunia nzima, hivyo Serikali haina mpango wa kufuta hati inayoridhisha yenye maoni ya kikaguzi wala kuingilia namna taaluma ya ukaguzi nchini inavyoendeshwa. Kutoa utaratibu mwingine itakuwa ni kukiuka Viwango vya Kimataifa vya Uandaaji wa Tarifa za Fedha katika Sekta ya Umma na pia Viwango vya Kimataifa vya Ukaguzi ambavyo Taifa na Serikali yetu imeviridhia vitumike.