Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 1 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 6 2020-01-28

Name

Dr. Ally Yusuf Suleiman

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mgogoni

Primary Question

MHE. ALLY SALEH ALLY (K.n.y. MHE. DKT. SULEIMANI ALLY YUSSUF) aliuliza:-

Kutokana na maendeleo ya kiuchumi na kijamii kumekuwa na ongezeko kubwa la makosa katika jamii jambo ambalo linasababisha mfumo wa utoaji haki pamoja na Mahakama kuelemewa.

(a) Je, kila Jaji au Hakimu anapangiwa kesi ngapi kwa mwaka ili kupunguza mlundikano wa kesi?

(b) Je, ni mambo gani kimsingi yanayosababisha mashauri kuchukua muda mrefu?

Name

Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Suleimani Ally Yussuf, Mbunge wa Mgogoni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania imejiwekea utaratibu ili kuhakikisha mashauri yote yanayofunguliwa Mahakamani yanamalizika kwa wakati. Utaratibu huu ni pamoja na kujiwekea malengo ya idadi ya mashauri yatakayoamuliwa na Jaji na Hakimu kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, malengo ni kuhakikisha tunapunguza mlundikano wa mashauri Mahakamani ambapo kwa mwaka kila Jaji anatakiwa kumaliza mashauri 220; Mahakimu katika Mahakama za Hakimu Mkazi wa Wilaya kumaliza mashauri 250 na katika Mahakama za Mwanzo 260.

Mheshimiwa Spika, pia Mahakama imejiwekea ukomo wa muda wa mashauri kukaa Mahakamani. Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu ni miaka mwili; Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya mwaka mmoja na Mahakama za Mwanzo ni miezi sita. Mikakati hii imesaidia kupunguza mlundikano wa mashauri kwa kiasi kikubwa hususan kwa Mahakama za Mwanzo ambapo kwa sasa mlundikano wa mashauri ni asilimia sifuri.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo bado Mahakama zetu zimekuwa zinakabiliwa na changamoto za mlundikano wa mashauri na baadhi ya mashauri kuchukua muda mrefu zaidi. Changamoto hizi zimetokana na idadi ndogo ya Majaji na Mahakimu ikilinganishwa na idadi ya mashauri yanayofunguliwa katika Mahakama zote nchini. Vilevile upelelezi katika Mahakama na mashauri kuchukua muda mrefu na mashahidi kutotoa ushahidi wao kwa wakati katika baadhi ya mashauri yanayofunguliwa katika Mahakama zetu nchini ni miongonzi mwa sababu na baadhi ya mashauri kuchukua muda mrefu Mahakamani. Hata hivyo ninamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa kuteuwa Majaji 11 wa Mahakama ya Rufaa na Majaji 39 wa Mahakama Kuu katika Awamu ya Tano, ahsante.