Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 1 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 12 2019-09-03

Name

Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi)

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA (K.n.y MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI) aliuliza:-

TPB ni Benki ya Serikali na inamilikiwa na Serikali kwa zaidi ya asilimia 90 lakini Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma yanatumia Benki nyingine katika huduma za Kibenki:-

(a) Je, ni nini msimamo wa Serikali katika kutumia huduma za Kibenki?

(b) Watumishi wa Serikali na Viongozi wote wa Serikali wanatakiwa kutumia TTCL katika huduma za mawasiliano ya simu. Je, kwa nini Watumishi na shughuli zote za Serikali zisianze kutumia huduma za Kibenki kupitia Benki hiyo?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu
(a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, biashara huria ya sekta ya fedha ilianza tangu mwaka 1991 mara baada ya kupitishwa kwa Sheria ya Benki na Taasisi za Fedha ya mwaka 1991, pamoja na Kanuni zake. Kupitia sheria hiyo, Wawekezaji mbalimbali walifungua Benki binafsi hapa nchini na hivyo matumizi ya huduma na bidhaa za benki kuanza kuamuliwa na nguvu ya soko ikiwa ni pamoja na huduma na bidhaa za Benki za Serikali. Benki ya TPB, kama ilivyo kwa benki nyingine haina budi kujiimarisha na kujitangaza yenyewe kwa lengo la kuuza bidhaa zake na hatimae kuvutia wateja zaidi ikiwa ni pamoja na Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia misingi ya nguvu ya soko, Benki ya TPB imefanikiwa kujitangaza na kuimarisha huduma zake na hivyo kuvutia baadhi ya Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma kutumia bidhaa zake. Miongoni mwa huduma za benki ya TPB zinazotumiwa na Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma kwa sasa ni pamoja na akaunti ya muda maalumu, akaunti ya biashara, malipo kwa njia ya mtandao, kubadilisha fedha za kigeni, kukusanya mapato ya Serikali, kulipa mishahara ya watumishi, mikopo kwa watumishi, kulipa pensheni za wastaafu pamoja na mikopo kwa wastaafu wanaolipwa pensheni zao na Serikali pamoja na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

(b) Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sera, Sheria, Kanuni, Taratibu na miongozo iliyopo ya uchumi huria, Serikali haina Mamlaka ya kumlazimisha Mtumishi au Taasisi ya Umma kutumia huduma za benki yoyote, ikiwemo benki ya TPB. Hivyo basi, ni jukumu la Benki ya TPB na benki nyingine kuboresha mifumo ya huduma na bidhaa zao ili kuvutia Watumishi wa Umma, pamoja na Taasisi za Umma kuanza au kuendelea kutumia huduma zao.