Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 27 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 223 2019-05-14

Name

Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, Serikali inatumia Sheria ipi kutowapa wafanyakazi stahiki zao zinazohusu kupandishwa madaraja na ongezeko la mwaka (Annual Increment) kwa wakati?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Barua ya Katibu Mkuu – Utumishi yenye Kumbukumbu Namba CAC. 45/257/01/E/83 ya tarehe 9 Septemba, 2013 kuhusu upandishwaji wa vyeo kwa madaraja kwa watumishi wote nchini wa umma huzingatia vigezo muhimu sana kama vile sifa za kitaaluma, uzoefu wa kazi, utendaji mzuri wa kazi kwa maana ya OPRAS, tange au ukubwa kazini kwa maana ya Seniority, uwepo wa ikama na bajeti iliyoidhinishwa kwa mwaka husika wa fedha, vilevile bila kusahau nidhamu na mwenendo wa mtumishi huyo wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ile ya E. 9(1) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, Toleo la Tatu, nyongeza ya mwaka ya mishahara haipaswi kuombwa au kudaiwa na watumishi wa umma bali Serikali ndio yenye uamuzi wa kutoa au kutokutoa nyongeza hiyo. Hivyo, katika utumishi wa umma hakuna sheria inayoainisha kwamba, mtumishi anatakiwa kupata nyongeza ya kawaida ya mshahara kwa kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ya E.2 ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 viwango vya mshahara ikiwa ni pamoja na nyongeza ya mshahara kwa kila mwaka kwa maana ya annual increment hupangwa kulingana na uwezo wa Serikali kulipa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitoa nyongeza ya mshahara ya kila mwaka kwa maana ya annual increment kwa watumishi wote wa umma kuanzia mwezi Novemba, 2017. Vilevile Serikali imewaelekeza waajiri wote kuendelea na upandishwaji vyeo kwa watumishi 193,166 waliokasimiwa katika ikama ya bajeti ya mwaka 2017/208 kuanzia tarehe 1 Mei, 2019 na barua zinaendelea kuingizwa kwenye mfumo wa taarifa za kiutumishi na mishahara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahimize watumishi wote wa umma kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kuleta tija katika utumishi wa umma na Serikali itaendelea kutoa nyongeza ya mshahara pamoja na kuboresha mazingira ya kazi kadri uwezo wa Serikali kulipa utakavyoruhusu. Ahsante.