Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 26 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 213 2019-05-13

Name

Ussi Salum Pondeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chumbuni

Primary Question

MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-

Viongozi wa Kitaifa wanaofanya ziara Tanzania walikuwa wakifika Zanzibar na kuonana na Rais wa Zanzibar:-

(a) Je, kwa nini katika siku za karibuni viongozi hao wamekuwa wakiishia Tanzania Bara?

(b) Je, ni viongozi wangapi wa Kimataifa ikiwemo Marais ambao wamefanya ziara Tanzania katika kipindi cha 2016/2017 na nchi wanazotoka?

(c) Je, kati ya viongozi hao wangapi wamefika Zanzibar na wangapi hawakufika na kwa sababu gani?

Name

Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza Mbunge wa Chumbuni len ye kipengele (a), (b) na (c) kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, kwa kawaida viongozi wa Kitaifa wanapokuja nchini wanakuwa na ratiba ya maeneo ambayo wameyaainisha kuyatembelea kulingana na muda waliopanga kuwepo nchini. Pamoja na hilo Wizara imekuwa ikiwashauri viongozi hao kuzuru maeneo m balimbali ya nchi hususan Zanzibar ili pamoja na mambo mengine kukutana na kufanya mazungumzo rasmi na viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi Aprili, 2019 jumla ya viongozi 21 wa Kimataifa walitembelea Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Viongozi hawa walitoka katika nchi za Afrika Kusini, Burundi, Chad, Cuba, Ethopia, India, Jamhuri ya Democrasia Congo, Jamhuri ya Korea, Msumbuji, Morocco, Mauritius, Misri, Malawi, Rwanda, Uturuki, Uganda, Vietnam, Sudan Kusini, Sri Lanka, Switzerland, Zambia na Zimbabwe.

Mheshimiwa Spika, kati ya viongozi hao wa Kimataifa waliotembelea Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tisa walifika Zanzibar na 12 kati yao hawakufika Zanzibar. Sababu zinazopelekea kutofika kwao ni kutokana na aina ya ziara, ratiba ya ziara husika na ufinyu wa muda katika ziara. Sababu nyingine ni vipaumbele na malengo ya ziara za viongozi hao pamoja na utashi wa kiongozi husika. Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeendelea kushauri viongozi wa Kitaifa kutoka nchi za kigeni wanaozuru nchini kutembelea Zanzibar katika ratiba zao. Aidha, Wizara kupitia Idara ya Mambo ya Nje Zanzibar imekuwa ikifanya maandalizi stahiki ya kiitifaki ili kurahisisha viongozi hao kutembelea Zanzibar.