Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 25 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 202 2019-05-10

Name

Zainabu Mussa Bakar

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR aliuliza:-

Walimu wote nchini wameingia katika Mkataba na Mwajiri ambao pamoja na mambo mengine unaonesha uwepo wa increment kila ifikapo mwezi Julai; tangu iingie madarakani Serikali ya Awamu ya Tano Walimu hawajapewa stahiki hiyo.

Je, ni lini Walimu watalipwa stahiki hiyo kama malimbikizo au haki hiyo imeshapotea?

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA - MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza miongozo mbalimbali iliyowekwa kuhusu maslahi ya walimu ikiwa ni pamoja na kutoa nyongeza za mwaka za mishahara kulingana na utendaji mzuri wa kazi na kwa kuzingatia tathmini ya utendaji kazi ya kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa kanuni E.9(1) ya kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 Toleo la Tatu, Nyongeza ya Mwaka ya Mishahara haipaswi kuombwa au kudaiwa na Walimu, bali Serikali ndiyo yenye uamuzi wa kutoa au kutotoa nyongeza hiyo kutokana na Sera za kibajeti kwa mwaka husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watumishi wa Umma wakiwemo walimu wanastahili kupewa nyongeza ya mwaka ya mshahara iwapo bajeti ya mishahara inaruhusu. Kutokana na ufinyu wa bajeti, nyongeza hiyo haikutolewa kwa watumishi katika mwaka wa fedha 2003/2004, 2004/2005, 2008/2009, 2011/2012, 2012/2013 na 2016/2017. Hata hivyo,
kwa kutambua utendaji mzuri wa kazi, Serikali ya Awamu ya Tano ilitoa nyongeza ya mwaka ya mshahara kwa watumishi wote wakiwemo walimu katika mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kutoa nyongeza ya mwaka ya mshahara kwa watumishi wote kadri uwezo wa kulipa utakavyoruhusu. Hata hivyo, walimu hawapaswi kudai malimbikizo ya nyongeza ya mwaka ya mshahara kwa miaka ambayo nyongeza hiyo haikutolewa. Ahsante.