Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 25 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 201 2019-05-10

Name

Hasna Sudi Katunda Mwilima

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kigoma Kusini

Primary Question

MHE. HASNA S. MWILIMA aliuliza:-

Jiografia ya Halmashauri ya Uvinza ni mbaya na kusababisha wanafunzi wanaomaliza Kidato cha Nne kutoka mwambao wa Ziwa Tanganyika kusafiri zaidi ya kilometa 200 kufuata Shule za Kidato cha Tano na Sita zilizopo katika ukanda wa Reli:-

(a) Je, kwa nini Serikali isianzishe Shule za Kidato cha Tano na Sita kwenye Kata nane za Ukanda wa Ziwa Tanganyika ili kuwapunguzia usumbufu wanafunzi hao?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati na kuongeza miundombinu katika Shule za Kidato cha Tano na Sita Rugufu Wasichana na Wavulana ambazo miundombinu yake ni chakavu na haitoshelezi?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Katumba Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza inaundwa na Tarafa tatu za Nguruka, Ilagala na Buhingu. Shule za Sekondari za Kidato cha I – IV ziko 20 (18 za Serikali na 2 za binafsi) zote zikiwa na jumla ya wanafunzi 11,622. Shule za Kidato cha Tano na Sita zipo tatu ambazo ni Lugufu Wavulana, Lugufu Wasichana, zote za Tarafa ya Nguruka na Kalenge iliyopo Tarafa ya Ilagala.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uanzishaji wa Shule za Kidato cha Tano na Sita ni la kisera, lakini Serikali inaendelea kuboresha na kupanua miundombinu katika Shule za Sekondari Buhingu katika Tarafa ya Buhingu na Sunuka katika Tarafa ya Ilagala ambazo zinatarajiwa kupandishwa hadhi na kuanza kutoa elimu ya Kidato cha Tano na Sita ifikapo Julai, 2020.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Shule za Sekondari za Lugufu Wavulana na Wasichana ni miongoni mwa Shule za Sekondari zilizoanzishwa kwenye maeneo yaliyokuwa Makambi ya Wakimbizi Mkoani Kigoma. Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri imekuwa ikitumia mapato ya ndani ya Halmashauri na kukamilisha vyumba vitatu vya maabara za Sayansi.

Vile vile Serikali Kuu kupitia progrmu ya EP4R imepeleka fedha za ukarabati wa matundu manane ya vyoo na shilingi milioni 150 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili mapya kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania.