Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 24 East African Co-operation and International Affairs Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 199 2019-05-09

Name

Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Primary Question

MHE. OTHMAN OMAR HAJI aliuliza:-

Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu (ACPHR) inatumia jengo la TANAPA lililopo Arusha kwa mkataba wa upangaji baina ya TANAPA na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ulioanza tarehe 1 Desemba, 2008 kwa kodi ya dola za Marekani 38,998.89 kwa mwezi:-

Je, kati ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu ni nani mwenye jukumu la haki za binadamu na nani mwenye jukumu la kulipa kodi ya jengo hilo?

Name

Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando, kama yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo mwaka 2007, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Umoja wa Afrika Mashariki ziliingia Mkataba wa Uenyeji (Host Agreement) wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Katika mkataba huo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano ndiyo msimamizi na mtekelezaji mkuu wa mkataba huo kwa niaba ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 5(1) ya mkataba kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Umoja wa Afrika Kuhusu Uenyeji wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, inaeleza kuwa Tanzania kwa gharama zake inawajibika kutoa majengo kwa ajili ya ofisi ya mahakama na makazi ya Rais na Msajili wa Mahakama hiyo. Aidha, Ibara ya 5(2) inaipa Tanzania jukumu la kutoa ofisi ya muda kwa ajili ya mahakama husika wakati ikiendelea na taratibu za kupata jengo la kudumu la mahakama. Kutokana na kipengele hicho Serikali iliingia mkataba na TANAPA wa kukodisha majengo yale ili kuwa ofisi ya muda ya Mahakama ya Haki za Binadamu na Watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maelezo hayo, ni dhahiri kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ndiyo yenye jukumu la kulipa kodi hiyo kutokana na makubaliano yaliyofikiwa. Hata hivyo, suala la kulinda haki za binadamu ni suala la kila mtu na kila taasisi sehemu yoyote duniani. Kimsingi, hata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inahusika moja kwa moja katika kulinda haki za binadamu.