Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 23 Water and Irrigation Wizara ya Maji 194 2019-05-08

Name

Peter Ambrose Lijualikali

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Kilombero

Primary Question

MHE. PETER A. LIJUALIKALI aliuliza:-

Je, kwa nini Serikali isifute kodi kwenye vifaa vya kusambazia maji kutokana na matatizo ya maji tuliyonayo katika Taifa letu?

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Peter Ambrose Lijualikali, Mbunge wa Jimbo la Kilombero, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tarehe 12 Septemba, 2017, Bunge lako Tukufu lilipitisha marekebisho ya Sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani, Sura ya 148. Marekebisho ya Sheria hiyo ya VAT yalihusisha vifungu vya 6 na 7 pamoja na aya ya 9 ya sehemu ya pili ya Jedwali la Sheria ya VAT ambayo vina lengo la kupunguza gharama za utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuongeza tija ya matumizi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi inayotekelezwa kwa fedha za Serikali na za washirika wa maendeleo inakamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maji tayari imeshasambaza Waraka wa Hazina namba sita uliotolewa na Wizara ya Fedha na Mipango kuhusu utaratibu wa kutoa msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa miradi ya maji itakayotekelezwa kote nchini. Ni wajibu kwa Maafisa Masuuli wote kuzingatia utaratibu ulioainishwa na Serikali katika misamaha ya kodi kwa vifaa vya kusambazia maji ili miradi yetu ya maji ikamilike kwa wakati.