Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 22 Energy and Minerals Wizara ya Madini 185 2019-05-07

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-

Je, ni lini uzalishaji wa madini ya Niobium utaanza katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali, niungane na Watanzania wote kuwatakia kheri Waislam wote katika Mfungo wa Ramadhani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Uchimbaji wa Madini ya Niobium unaomilikiwa na Kampuni ya Panda Hill Mines Limited, kampuni hii ina ubia na kampuni ya Cradle Resources Limited asilimia 50 na Tremont Investment asilimia
50. Kampuni hiyo inamiliki leseni tatu za Uchimbaji wa Kati wa Madini Na.237, 237 na 239 za mwaka 2006 zilizotolewa tarehe 16 Novemba, 2006 zikiwa na jumla ya kilomita za eneo la mraba 22.1. Mradi utausisha uchimbaji wa madini ya Niobium ambayo yataongezewa thamani kwa kuchanganywa na madini ya chuma na kuwa Ferro-Niobium, zao ambalo litauzwa kwa wanunuzi mbalimbali walioko Ulaya, Asia na Amerika ya Kaskazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji ameshafanya upembuzi yakinifu (feasibility study) uliokamilka mwaka 2016 na kujiridhisha uwepo wa mashapo ya kutosha utakaowezesha uhai wa mgodi huo ambao utadumu kwa takribani miaka 30. Hata hivyo, kufuatia mabadiliko ya Sheria ya Madini ya Mwaka 2017, mwekezaji alilazimika kupitia upya na kurekebisha taarifa za upembuzi yakinifu ili kuzingatia viwango vipya vya mrabaha, kodi na hisa za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, mwekezaji amewasilisha andiko la mradi la kuomba ufafanuzi wa vipengele mbalimbali kwa sheria na kutoa mapendekezo yake juu ya utekelezaji wa mradi huo, pamoja na suala la fidia ya ardhi kwa Gereza la Mbeya ambalo linatakiwa kuhamishwa ili kupisha mradi huo. Baada ya kupokea andiko hilo, hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwemo majadiliano na mwekezaji ambapo Wizara inatarajia kutoa mapendekezo yatakayowezesha kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo.