Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 21 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 167 2019-05-06

Name

Vedastus Mathayo Manyinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE. VEDASTUS M. MANYINYI aliuliza:-

Serikali katika kuhakikisha inapata watumishi bora na wenye sifa iliamua kuwaondoa watumishi wasio na sifa pamoja na wenye vyeti feki, lakini zoezi hilo lilikumbwa na changamoto mbalimbali ambapo Afisa Utumishi aliwaondoa watumishi kwenye payroll bila sababu maalum na walipofuatilia Wizarani walirudishwa kazini:-

(a) Je, kwa nini Serikali isiunde timu maalum ili ipite kila Halmashauri kupitia taarifa juu ya zoezi hili ili haki itendeke hasa kwa wale ambao hawana uwezo wa kwenda Wizarani?

(b) Wapo watumishi ambao baada ya kuajiriwa kwa kutumia vyeti feki walijiendeleza kielimu zaidi ya Darasa la Saba na wameondolewa kwa kosa la udanganyifu wa vyeti: Je, Serikali haioni kuwa hao ni bora kuliko wale ambao hawakujiendeleza?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kushirikiana na waajiri na Baraza la Mitihani la Taifa, Serikali iliendesha zoezi maalum la kuhakiki vyeti vya ufaulu mtihani wa Kidato cha Nne, Kidato cha Sita na Ualimu. Kupitia zoezi hilo, watumishi 15,189 walibainika kuwa na vyeti vya kugushi na kuondolewa kwenye orodha ya malipo ya mshahara (payroll).

Hata hivyo, baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa watumishi na vyanzo vingine kuhusu watumishi kuondolewa kimakosa au kwa uonevu katika orodha ya malipo ya mishahara, Serikali imekuwa ikifanya ufuatiliaji wa karibu ikiwa ni pamoja na kuunda timu za ufuatiliaji wa utekelezaji wa zoezi hili. Jumla ya watumishi 4,160 waliobainika kuondolewa kimakosa au kwa uonevu wamerejeshwa kazini. Kati ya watumishi waliorejeshwa kazini 3,057 ni Watendaji wa Vijiji/Mtaa na Kata.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi wanaojiendeleza zaidi ya Darasa la Saba wanafanya vizuri na Serikali inahimiza watumishi kujiendeleza kielimu. Hata hivyo, kwa mujibu wa Kanuni ile ya D.12 ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, ni makosa kwa mtumishi kujipatia ajira kwa njia ya udanganyifu.

Hivyo Serikali ilielekeza waajiri kuwaondoa kwenye orodha ya malipo ya mishahara Watumishi wa Umma wote walioajiriwa kabla ya tarehe 20, Mei, 2004 ambao katika kumbukumbu zao rasmi za kiutumishi walijaza taarifa za udanganyifu kwamba walifaulu mitihani ya Kidato cha Nne, lakini hawakuthibitisha taarifa zao kwa kuwasilisha vielelezo vya sifa hizo kama vile taarifa binafsi (personal records).

Hivyo, pamoja na watumishi hao kujiendeleza kielimu, uamuzi wao wa kutoa taarifa za udanganyifu unawaondolea sifa ya uaminifu na uadilifu kwa Serikali na hivyo wanakosa sifa za kuendelea kuwa Watumishi wa Umma. Ahsante.