Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 16 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 133 2019-04-25

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:-

Je, kwa nini Serikali inatenga na kutumia fedha kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vitongoji na Vijiji?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, tuna majibu yake. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba nimjibu Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, madhumuni ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kama ilivyotajwa kwenye Katiba, Ibara ya 146(2)(a) mpaka (c) ni kuimarisha demokrasia na kutumia demokrasia katika kuharakisha maendeleo. Katika kutekeleza jukumu hili muhimu, viongozi wanaoongoza vyombo vya Serikali za Mitaa huchaguliwa kwa njia ya kidemokrasia kupitia uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika ngazi ya vijiji, mitaa na vitongoji.

Mheshimiwa Spika, uchaguzi wa Serikali za Mitaa unahitaji rasilimali fedha ili kuwezesha upatikanaji wa mahitaji mbalimbali kwa ajili ya uchaguzi ikiwemo vifaa vya uchaguzi yani masanduku, lakiri, fomu na kadhalika. Pamoja na vifaa hivyo, zipo gharama mbalimbali zinazohusiana na uendeshaji wa uchaguzi huo ikiwemo mafuta ya magari, matengenezo ya magari na posho mbalimbali kwa ajili ya watu watakaoshughulikia mchakato mzima wa uchaguzi.

Mheshimiwa Spika, vilevile zipo taratibu za kisheria ambazo zinapaswa kufuatwa katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa kama vile kutoa matangazo ya Kiserikali yanayohusu uchaguzi, kufanya vikao mbalimbali na wadau wa uchaguzi, kuhakiki maeneo au majimbo ya uchaguzi na kuandaa Daftari la Wapiga Kura, kuratibu shughuli hizo zote zinahitaji rasilimali fedha. Hivyo, kukamilisha Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni lazima Serikali itenge fedha za kugharamia shughuli hizo, kama ilivyo kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani. Ahsante.