Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 12 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 106 2019-04-17

Name

Juma Selemani Nkamia

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chemba

Primary Question

MHE. JUMA S. NKAMIA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Chemba?

Name

Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Wilaya ya Chemba ni moja ya wilaya zinazokabiliwa na ukosefu wa huduma za mahakama ya wilaya. Kwa nyakati tofauti, nimekuwa nikilieleza Bunge lako Tukufu kwamba Mahakama ya Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa ya miundombinu ya kutolea huduma za kimahakama katika ngazi zote. Kati ya Wilaya 139 zilizopo nchini, ni Wilaya 34 tu zenye majengo ya mahakama.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Mahakama ya Tanzania imekuwa ama ikiazima majengo kwenye Ofisi za Halmashauri, Mkuu wa Wilaya au kupanga pale yanapokosekana kabisa majengo hayo, ili kuendelea kutoa huduma za kimahakama. Katika maeneo ambayo Mahakama ya Tanzania haina kabisa majengo huduma hiyo imekuwa ikiendelea kutolewa na mahakama ya wilaya nyingine iliyopo jirani kwa utaratibu wa kuitembelea kwa ratiba walizojipangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uhaba wa miundombinu takribani wilaya mpya 29, ikiwemo ya Chemba mkoani Dodoma ambayo imetokana na Wilaya ya Kondoa bado haina Mahakama ya Wilaya. Hivyo, Wilaya hiyo kwa sasa inaendelea kuhudumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Kondoa. Hata hivyo, katika mwaka wa fedha 2019/2020, mpango wa Mahakama ya Tanzania ni kuhakikisha kuwa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Chemba linajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa lengo la Serikali ni kusogeza huduma za mahakama karibu na wananchi, naomba kumthibitishia Mbunge kwamba tutafanya kila jitihada ya kuendeleza ujenzi wa mahakama kila wilaya hapa nchini inapokuwa inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.