Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 7 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 61 2019-04-10

Name

Fatma Hassan Toufiq

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-

Miongoni mwa sababu kubwa zinazosababisha wanawake na watoto kuporwa mali zao na ndugu za waume zao ni kukosekana kwa wosia, jambo ambalo jamii haijaona umuhimu huo wakiamini kuwa kuandika wosia ni kujitakia kifo:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani endelevu wa kukabiliana na kadhia hii?

(b) Je, Serikali itakuwa tayari kuielimisha jamii umuhimu wa kuandika wosia kama njia mojawapo ya kulikabili tatizo hili ambalo ni kubwa katika jamii?

Name

Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuandika wosia kama njia mojawapo ya kukabiliana na migogoro katika jamii inayohusiana na mgao wa mali za marehemu. Kwa kutambua hilo, mwaka 2008, Wizara yangu kupitia Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi (RITA) iilianzisha huduma ya kuandika na kuhifadhi wosia ikiwa ni pamoja na kuuelimisha umma kuhusiana na huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu wakati huo, Wizara yangu kupitia Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi inaendelea kubuni na kutekeleza mikataba ya aina mbalimbali ili kuhakikisha na kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuandika na kuhifadhi wosia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukitumia njia mbalimbali kutoa elimu ya kuandika wosia ikiwa ni pamoja na mikutano ya hadhara, redio, televisheni, vipeperushi, magazeti na mitandao ya kijamii. Pamoja na jitihada hiyo, mpaka sasa tumeweza kuandika na kuhifadhi wosia 578 kati ya hizo 32 tayari zimeshatumika. Hata hivyo, idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na idadi kubwa ya Watanzania waliopo kwa sasa. Bado kuna changamoto ya uelewa kwa wananchi wengi juu ya umuhimu wa suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kulithibitishia Bunge lako Tukufu kuwa Wizara yangu itaendelea kubuni njia mbalimbali za kuelimisha jamii kuwa umuhimu wa kuandika wosia ikiwa ni jitihada mojawapo ya kukabiliana na migogoro ya mgao wa mali za marehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba kutumia fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote kuchangia katika juhudi zinazofanywa na Serikali za kuhamasisha wananchi kujijengea tabia na utamaduni wa kuandika na kuhifadhi wosia sehemu maalum hadi utakapohitajika. Endapo wananchi watahamasika, tutakuwa tumeondokana na migogoro isiyo ya lazima na hivyo kuruhusu maendeleo ya ustawi wa jamii. Hii ni njia muhimu ya kulinda haki za wanawake na watoto waliofiwa ndani ya familia.