Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 5 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 38 2019-04-08

Name

Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ALLY K. MOHAMED (K.n.y. MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa shamba la Efatha Mkoani Rukwa?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu wa matumizi ya Shamba Na. 48/1 la Malonje kati ya mmiliki ambaye ni Mdhamini wa Efatha na wananchi wa vijiji vinavyozunguka shamba hili, hususan Vijiji vya Songambele, Sikaungu na Msanda Muungano. Madai ya wananchi hao ni kuwa sehemu ya shamba hili imeingia ndani ya vijiji vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo awali Shamba la Malonje lilikuwa likimilikiwa na Wizara ya Maji na Maendeleo ya Mifugo likiwa halina upimaji ambapo lilipimwa mwaka 1997 likiwa na ukubwa wa hekta 15,000. Mwaka 2007 shamba hili liligawanywa ambapo hekta 10,000 ziliuzwa kwa wamiliki ambao ni Efatha Ministry na hekta 5,000 zilizobaki zilipimwa vitalu na kugawiwa wafugaji. Mwaka 2010 baada ya kupokea malalamiko na kuyafanyia kazi, ilibainika kuwa upimaji wa vijiji uliofanyika umeingiliana na mipaka ya shamba husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga na Mkoa wa Rukwa, imefanya jitihada mbalimbali za kumaliza mgogoro huo. Baada ya jitihada hizo kutozaa matunda, tarehe 7 Novemba, 2017 nilikutana na Mwenyekiti wa Bodi ya Huduma ya Efatha na baadhi ya Watendaji wake kwa lengo la kukubaliana namna bora ya kumaliza mgogoro huu ili kuboresha mahusiano ya ujirani mwema kati ya mmiliki na wananchi wa vijiji vinavyozunguka shamba hilo. Wizara yangu ilipendekeza kwamba Efatha iridhie kuachia sehemu ya ardhi ya shamba yenye ukubwa wa ekari 8,392.9 na kuigawa kwa wananchi wa vijiji husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Bodi ya Wadhamini kukaa, waliridhia kutoa ekari 3,000 kwa Vijiji vya Songambele, Sikaungu na Msanda Muungano kwa maana ya kila kijiji kigawiwe ekari 1,000. Hata hivyo, Kijiji cha Sikaungu kimekataa kupokea ekari hizo kwa kuwa wao wanataka kiasi cha ardhi kama ilivyoonekana kwenye vyeti vyao vya ardhi ya kijiji.

Aidha, majadiliano bado yanaendelea kati ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Efatha na Serikali ya Kijiji cha Sikaungu. Baada ya majadiliano hayo kukamilika, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Halmashauri itasimamia upimaji wa ardhi hiyo.