Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 5 Enviroment Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano 37 2019-04-08

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-

Matumizi ya mifuko ya plastiki hapa nchini yamekuwa na athari kubwa kwenye uharibifu wa mazingira na uchafuzi wa miji yetu:-

Je, Serikali ina mikakati gani ya kuondoa matumizi ya plastiki hapa nchini?

Name

Mussa Ramadhani Sima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa matumizi ya mifuko ya plastiki yameongezeka hasa kutokana na mifuko hii kutolewa bure kwenye maduka, masoko, migahawa na maeneo mbalimbali. Aidha, kutokana na baadhi ya nchi jirani kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki na kuruhusu uzalishaji kwa ajili ya soko la nje ya nchi, kumekuwa na wimbi kubwa la uingizaji wa mifuko ya plastiki nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia hali hii na mwelekeo wa Jumuiya ya Kimataifa wa kudhibiti uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka za plastiki, Serikali inadhamiria kusitisha uzalishaji na matumizi ya mifuko ya plastiki katika siku zijazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, imeanza kuchukua hatua zifuatazo katika kuelekea kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki:-

(a) Kuhamasisha wajasiriamali, vikundi vya akinamama na vijana, sekta binafsi na viwanda kuwekeza katika uzalishaji wa mifuko mbadala ikiwemo vikapu vya asilia, mifuko ya karatasi na vitambaa;

(b) Ofisi imeendesha mikutano miwili ya wadau katika Mikoa ya Dar es Salaam tarehe 6 Novemba, 2018 na Mwanza tarehe 18 Novemba, 2018, kuelimisha umma kuhusu changamoto na athari za mifuko ya plastiki na kuhamasisha uwekezaji katika uzalishaji wa mifuko mbadala kutokana na dhamira ya Serikali kusitisha matumizi ya mifuko ya plastiki katika siku zijazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mikutano hii, wadau na wananchi waliishauri Serikali kuchukua hatua za haraka kudhibiti matumizi ya mifuko ya plastiki na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji katika uzalishaji wa mifuko mbadala.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, napenda kuchukua fursa hii, kwa mara nyingine tena kuhimiza viwanda vinavyozalisha mifuko ya plastiki na wadau wengine kujitayarisha kwa kubadili teknolojia na kutathmini fursa zinazojitokeza katika kuzalisha mifuko mbadala hasa katika kipindi hiki cha mpito wakati taratibu za maamuzi ya Serikali zikikamilishwa.