Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 4 Industries and Trade Wizara ya Viwanda , Biashara na Uwekezaji 27 2019-04-05

Name

Mussa Bakari Mbarouk

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Tanga Mjini

Primary Question

MHE. SONIA J. MAGOGO (K.n.y. MHE. MUSSA B. MBAROUK) aliuliza:-

Wakazi wa Kata ya Kirare, Tongoni, Mzizima, Chongoleani, Mabokweni na Pongwe Wilayani Tanga Mjini ni wazalisaji wakubwa wa zao la muhogo lakini hawana soko la uhakika:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutafuta soko la uhakika wa zao la muhogo ndani na nje ya nchi?

(b) Zipo mashine za kuchakata muhogo lakini bei zake ni kubwa na hivyo wakulima hawana uwezo wa kununua; je, Serikali haioni haja ya kuondoa kodi katika mashine hizo?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, imeweka vipaumbele vitatu ambavyo ndivyo tunavyoviwekea msisitizo wa uwekezaji kwenye sekta ya viwanda. Vipaumbele hivyo ni viwanda vya kusindika mazao ya kilimo ili kuongeza thamani sambamba na kulinda jasho la mkulima; viwanda vya kutengeneza bidhaa za majumbanii kama vyakula, nguo, mafuta ya kula, samani na kadhalika na bidhaa tegemezi kwenye sekta ya ujenzi kama sementi, mabati na kadhalika ili kuharakisha ubora wa maisha na maendeleo; viwanda vinavyoajiri watu wengi kwa ajili ya kuhakikisha ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la muhogo ambalo ni maarufu kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Lindi, Mtwara na maeneo mengi ya nchi hadi Kigoma kwa sasa limepewa kipaumbele maalum duniani. Kutokana na ukweli kwamba muhogo hausindikwi kutengeneza unga wa ugali au uji au mkate au biskuti peke yake bali unga wa muhogo unatumika kwa sasa kwenye uunganishaji wa chuma, mbao, kutengeneza gundi na matumizi mengine mengi sana. Soko la muhogo Ulaya, Marekani na China ni kubwa sana kwa sasa. China peke yake inahitaji tani milioni mbili na nusu za muhogo kwa mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ukweli huo, kasi ya ujenzi wa viwanda vya kusindika muhogo ni kubwa. Mwaka huu peke yake ukiacha viwanda vitano vinavyonunua muhogo wa mkulima kwa sasa kikiwemo kile kilichopo Handeni, viwanda viwili vipya vitakuwa vimefunguliwa kabla ya Juni, 2019 kimoja Lindi na kingine Pwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu bei kubwa za mitambo kutoka nje, nawashauri wawekezaji wa ndani watembelee SIDO na TEMDO kwanza maana ni taasisi za ndani ambapo miongoni mwa majukumu yake ni kubuni na kutengeneza mitambo na mashine za kusindika mazao zenye gharama nafuu. Endapo italazimika kuagiza nje ya nchi, italazimu kufuata Sheria ya Fedha iliyopo au kusubiri mapendekezo yaliyopelekwa kwenye Kikosi Kazi cha kutathmini mapendekezo ya marekebisho ya kodi yatakayojadiliwa wakati wa kujadili rasimu itakayoletwa na Serikali Bungeni Juni, 2019.