Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 1 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 8 2019-04-02

Name

Ussi Salum Pondeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chumbuni

Primary Question

MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-

Wananchi wa Kisakasaka, Mkoani Mjini Magharibi Unguja wamekuwa na mgogoro wa ardhi wa muda mrefu na Kambi ya Jeshi la Wananchi na hivyo kuathiri shughuli zao za kiuchumi:-

(a) Je, Serikali imechukua hatua gani kumaliza mgogoro huo?

(b) Je, ni sababu gani zimesababisha mgogoro huo kudumu zaidi ya miaka 40?

(c) Je, ni lini Taasisi husika za Serikali zitakaa pamoja na kumaliza mgogoro huo?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Kambi ya Kisakasaka yenye ukubwa wa hekari 490 ilianzishwa mwaka 1978 lengo likiwa ni kulinda anga na Manispaa ya Mji wa Zanzibar na vituo muhimu. Eneo hilo liliwahi kupimwa mwaka 1985 lakini halikuwahi kupatiwa hatimiliki kwa sababu Sheria mpya ya Ardhi ya Zanzibar Na. 12 ya mwaka 1992 haikutambua upimaji uliofanywa kabla ya hapo. Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa inatambua uwepo wa mgogoro husika na imekuwa ikichukua hatua kadhaa kuumaliza kama ifuatavyo:-

(i) Mwaka 2013 fedha kiasi cha Sh.4,150,000/= kililipwa kwa Idara ya Upimaji na Ramani ya Zanzibar ili kufanya kazi ya upimaji na kuandaa hatimiliki. Kazi hii haijafanyika kwa sababu wananchi hawakuridhika na upimaji huo.

(ii) Katika muendelezo wa kumaliza mgogoro huo, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi alitembelea aneo hilo na kuridhia mipaka irekebishwe kwa kuzingatia maslahi mapana ya Jeshi na mahitaji ya ardhi kwa wananchi.

(b) Mheshimiwa Spika, baadhi ya sababu zilizopelekea mgogoro kudumu kwa muda mrefu ni kukosekana kwa fedha za kugharamia kazi za upimaji, uthamini na ulipaji fidia katika maeneo yaliyotwaliwa na Jeshi.

(c) Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imekubali kuunda Kikosi Kazi kitakachopitia maeneo yote yenye migogoro kwa Zanzibar ambacho kitatoa mapendekezo ya kudumu ya kumaliza migogoro hiyo.