Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 10 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 114 2019-02-08

Name

Amb. Adadi Mohamed Rajabu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muheza

Primary Question

MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-

Katika kijiji cha Fanusi, Kata ya Kisiwani, Wilayani Muheza wapo wananchi wanaofanya biashara ya kutega vipepeo na kuvipeleka nje ya nchi kwa ajili ya kupata kipato na pia njia ya kukuza utalii:-

(a) Je, ni lini wataruhusiwa kupeleka tena vipepeo nje ya nchi badala ya Serikali kuzuia kama ni wanyama hai?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuboresha maeneo hayo ili kuwavutia watalii waweze kuja kwa wingi?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajabu, Mbunge wa Jimbo la Muheza, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipepeo ni moja ya aina za wanyamapori waliokuwa wakifanyiwa biashara ya wanyamapori hai kwa kusafirishwa nje ya nchi kwa mujibu wa Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya Mwaka 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na wafanyabiashara kukiuka Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 na Kanuni zake; Serikali ilisitisha biashara ya kusafirisha wanyamapori hai nje ya nchi kwa muda wa miaka mitatu kuanzia Mei, 2016. Aidha, kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa, Serikali imeamua kuendelea kufunga biashara ya usafirishaji wanyamapori hai nje ya nchi. Kufuatia uamuzi huo, Wizara inaandaa namna bora ya kushughulikia wanyamapori waliopo kwenye mashamba/ mazizi. Aidha, wafanyabiashara walioathirika kutokana na zuio la kusafirisha wanyamapori nje ya nchi watarudishiwa fedha zao walizotumia kulipia Serikalini kwa ajili ya huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaboresha maeneo ya kuvutia watalii yaliyopo katika Hifadhi ya Msitu wa Mazingira Asilia wa Amani ambapo Kijiji cha Fanusi na vijiji vingine 20 vinapakana. Hifadhi hiyo ina vivutio vingi ikiwemo misitu minene, mito, wanyamapori na mimea adimu isiyopatikana maeneo mengine duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu huo, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania – TFS inatekeleza mpango wa kuendeleza utalii wa ikolojia na kiutamaduni katika hifadhi ya Amani. Mpango huu unahusu kuboresha miundombinu ikiwemo barabara ya kuelekea Msitu wa Amani, nyumba za kulala wageni zilizopo ndani ya msitu, vituo vya kupumzikia watalii (camp sites) na njia za watalii (nature trails). Juhudi hizi zinatarajiwa kuongeza idadi ya watalii, kuongezeka kwa biashara, fursa za ajira na uwekezaji kwa maeneo yaliyo karibu na msitu huo.