Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 8 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 96 2019-02-06

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-

Ardhi ni rasilimali ya msingi katika nchi yoyote duniani na tamaa ya kupora ardhi imesababisha migogoro na vita:-

(a) Je, Serikali ilitenga bajeti kiasi gani kuanzia mwaka 2010 – 2015 kwa ajili ya kupima matumizi ya ardhi?

(b) Je, kati ya kilometa za mrada 945,000 za Tanzania ni eneo kiasi gani limepimwa hadi Disemba 2015?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Ruth Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa nabu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi Namba 6 ya Mwaka 2007, uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi ni jukumu la mamlaka za upangaji ambazo ni Tume ya Taifa ya Upangaji wa Matumizi ya Ardhi kwa ngazi ya Taifa, Halmashauri za Wilaya pamoja na Halmashauri za Vijiji. Serikali imekuwa ikitenga fedha za kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka wa Fedha 2010 na 2011 hadi 2014/2015, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi ilitenga na kutumia kiasi cha shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kuandaa na kutekeleza mipango ya matumizi ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini. Aidha, wadau wa maendeleo wamekuwa wakiziwezesha mamlaka za uandaaji kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi imekuwa ikiboreshwa mwaka hadi mwaka. Kati ya mwaka 2015 hadi 2018 Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi ilitenga jumla ya shilingi bilioni 6.3 kwa ajili ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi nchini. Kati ya fedha hizi kiasi cha shilingi bilioni 1.3 kimetumika kati ya mwaka 2015/2016 na 2017/2018 na kiasi cha bilioni tano kimetengwa kwa bajeti ya Tume kwa Mwaka 2018/2019.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi ya Tanzania imegawanyika, katika aina tatu ambazo ni ardhi ya kawaida, ardhi ya hifadhi na ardhi ya vijiji. Hadi sasa kuna takribani vipande vya ardhi 2,000 vilivyopimwa ambavyo vinakadiriwa kuwa na ukubwa wa eneo la kilometa za mraba 141,750 sawa na asilimia 15 ya eneo la nchi. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi inaendelea na uboreshaji wa kumbukumbu za ardhi ikiwemo takwimu za upimaji ardhi kupitia mfumo unganishi wa kutunza kumbukumbu za ardhi, yaani ILMIS.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha kuwa eneo la ardhi ya nchi lililopimwa linaongezeka. Mojawapo ya mikakati hiyo ni mkakati wa kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi nchini ulioanza kutekelezwa mwaka 2016 kupitia programu mbalimbali ikiwemo Programu ya Kuwezesha Umilikishaji wa Ardhi, yaani Land Tenure Support Progamme, katika Wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi Mkoani Morogoro. Ni matarajio ya Wizara kuwa, kupitia mkakati huu idadi ya vipande vya ardhi vilivyopimwa itaongezeka na hivyo kupunguza eneo la nchi ambalo halijapimwa.