Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 7 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 77 2019-02-05

Name

Allan Joseph Kiula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Mashariki

Primary Question

MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-

Wakazi wa Jimbo la Mkalama wanapata shida sana kufuata huduma za Mahakama katika Wilaya ya Iramba – Kiomboi, umbali mrefu kutoka Mkalama:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya yalipo Makao Makuu ya Wilaya ya Mkalama?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuanzisha Mahakama ya muda ya Wilaya katika majengo ya Mahakama ya Mwanzo Nduguti?

Name

Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Iramba Mashariki, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama imejiwekea mkakati wa kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama kwa awamu, lengo likiwa ni kuwa na majengo katika wilaya zote ifikapo mwaka 2021. Katika mkakati huo, jengo la Mahakama ya Wilaya ya Mkalama limepangwa kujengwa mwaka 2019 na 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge kuhusu kutumia jengo la Mahakama ya Mwanzo Nduguti kuanzisha huduma za Mahakama ya Wilaya. Hata hivyo, tumefanya tathmini na kubaini kuwa jengo linalotumika sasa kwa Mahakama ya Mwanzo ya Nduguti halitoshelezi kuendesha Mahakama ya Wilaya na ya Mwanzo kwa kuwa mahitaji ya huduma za Mahakama za Mwanzo bado ni makubwa. Mpango tulionao ni kuanzisha Mahakama ya Wilaya katika Mahakama ya Mwanzo Iguguno, ujenzi wa jengo jipya katika Mahakama ya Mwanzo Iguguno umekamilika na kwa tathmini iliyofanyika linaweza kutumika kwa Mahakama ya Wilaya ya Mkalama na Mahakama ya Mwanzo Iguguno kwa muda wakati mipango ya kujenga ya ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tunaendelea kukamilisha taratibu za upatikanaji wa vifaa, watumishi, pamoja na taratibu za kisheria ili kuweza kuanzisha Mahakama hiyo kabla ya mwisho wa mwezi Juni, 2019.