Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 7 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 72 2019-02-05

Name

Janeth Maurice Massaburi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JANETH M. MASABURI aliuliza:-

Kumekuwa na upungufu wa rasilimali watu katika taasisi za umma na baadhi ya watumishi kushindwa kufanya maamuzi:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha kwa ajili ya mafunzo ndani na nje ya nchi kwa watumishi wa umma ili kuwajengea uwezo na kuleta tija kwa Taifa?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janeth Maurice Masaburi, Mbunge wa Kuteuliwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwapatia mafunzo watumishi wa umma ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi. Kwa kutambua hilo, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora huandaa sera, kanuni na miongozo inayohusiana na mafunzo katika utumishi wa umma na kufuatilia utekelezaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Menejimenti ya Ajira ya mwaka 1999 na marekebisho yake ya mwaka 2008 kifungu 4.8; Sera ya Mafunzo katika Utumishi wa Umma ya mwaka 2013 kifungu 4.2; na Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 kifungu G 1 (vifungu vidogo 7, 9, 10 na 11) zinasisitiza kuhusu umuhimu wa kila mwajiri katika utumishi wa umma kuandaa na kutekeleza Mpango wa Mafunzo kwa mujibu wa tathimini ya mahitaji ya mafunzo kwa maana ya (Training Needs Assessment).

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018 kupitia Wizara, Idara zinazojitegemea pamoja na Wakala, Serikali ilitenga jumla ya Sh.54,470,327,822 kwa ajili ya kugharamia mafunzo ya ndani na nje kwa watumishi wa umma. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, jumla ya Sh.39,839,347,632 zimetengwa kwa ajili hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wa maendeleo hususani Australia, India, Japan, China, Indonesia na Jamhuri ya Korea ambapo katika mwaka ule wa 2016/2017 kupitia wadau hao jumla ya watumishi wa umma 654 walipatiwa mafunzo ya muda mfupi na mrefu katika nchi hizo. Aidha, katika mwaka ule wa 2017/2018, fursa za mafunzo zilizotolewa na washirika hao ziliongezeka hadi kufikia 827. Fursa hizo zimewezesha watumishi wa umma kupata uelewa, ujuzi na maarifa mapya ya kumudu majukumu yao katika kutekeleza malengo ya Taifa. Ahsante.