Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
| Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
|---|---|---|---|---|---|---|
| 2015-2020 | Session 14 | Sitting 6 | Works, Transport and Communication | Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano | 59 | 2019-02-04 |
Name
Magdalena Hamis Sakaya
Sex
Female
Party
CUF
Constituent
Kaliua
Primary Question
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Mkandarasi aliyepewa tenda ya kujenga barabara ya lami kutoka Urambo kwenda Kaliua kilometa 28 ameonyesha udhaifu mkubwa katika kutekeleza kazi hiyo tangu awali:-
Je, kwa nini Serikali isisitishe mkataba wa mkandarasi huyo haraka kwa kumpata mkandarasi mwenye uwezo na uzoefu ili kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo muhimu kwa wakati na ubora?
Name
Elias John Kwandikwa
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ushetu
Answer
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mradi wa Ujenzi wa kwa kiwango cha lami wa barabara ya Urambo-Kaliua kilomita 28 ni moja kati ya miradi iliyotengwa mahsusi na Serikali kwa ajili ya wakandarasi wa ndani ili kuwajengea uwezo na kupata miradi mikubwa ya barabara. Mchakato wa kumpata mzabuni ulifanyika kwa malengo hayo.
Mheshimiwa Spika, aidha, muungano wa Wakandarasi watatu wazalendo, Salum Motor Transport Limited, Annam Road Works Company Limited na Jossam Company Limited walikidhi vigezo na hivyo kushinda zabuni hiyo. Utekelezaji wa mradi huu ambao unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 ulianza rasmi tarehe 30 Agosti, 2017 na muda wa utekelezaji ni miezi 26. Hadi sasa wakandarasi hawa wameendelea na kazi japo kwa kasi ndogo lakini kwa kiwango cha kuridhisha ambapo utekelezaji umefikia asilimia 35.
Mheshimiwa Spika, kasi ndogo ya utekelezaji ilichangiwa na mabadiliko ya hali ya hewa ambapo mvua nyingi ziliathiri utekelezaji ambapo mkandarasi ameomba kuongezewa muda. Hatua nyingine zinazochukuliwa na Serikali ni pamoja na kuhakikisha kuwa Mhandishi Mshauri wa mradi anaendelea kuwafundisha wakandarasi hawa kuhusu usimamizi wa miradi ili lengo lililopangwa liweze kufikiwa.
Mheshimiwa Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa kutokana na hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Seikali, mradi huu utakamilika kwa ubora na viwango vilivyopangwa kimkataba. Hivyo, kusitisha mkataba kwa hatua iliyofikiwa haitakuwa na tija kwa Serikali kwani tuna imani kuwa kutokana na mafunzo wanayoyapata wakandarasi hawa wazawa watakamilisha mradi huu kwa viwango vinavyotakiwa.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved