Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 6 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 58 2019-02-04

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Primary Question

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL aliuliza:-

Aliyekuwa Naibu Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Olenasha alitembelea Wilaya ya Siha kufuatilia ubadhirifu kwenye Shamba la Ganrangua na SACCOS ya Sanya Juu wa shilingi milioni 337 na Siha Kiyeyu shilingi milioni 840 ambapo aliiagiza TAKUKURU kuchunguza ubadhirifu huo:-

(a) Je, Serikali iko tayari kufanya upembuzi na kutambua mashamba ya umma, yasiyotumika vizuri na kurejesha kwa wananchi kwa kutumia vijiji na ushirika wao kama wazo la kwanza la Baba wa Taifa J. K. Nyerere, mfano wa baadhi ya mashamba hayo ni Kafoi Farm (Mifugo), Leoni(Ushirika-Mfilisi), Msingi (Ushirika-Mfilisi), Pirita (Ushirika- Mfilisi), Pongo (Ushirika-Mfilisi) na mengine mengi?

(b) Pamoja na juhudi nzuri zilizofanywa na Waziri Mkuu kuhusu ubadhirifu KNCU, je, Serikali ina taarifa kuwa ubadhirifu kwenye mali za KNCU na Vyama vya Ushirika ni mkubwa na unaendelea kulindwa na wahusika hawagusiki na bei ya zao la kahawa linaendelea kuathirika?

(c) Je, Serikali inaweza kuwaeleza nini wananchi wa Siha kuhusu Shamba la Gararagua lililouzwa na KNCU mwaka 2014 na makabidhiano kufanyika mwaka 2016, likitoka mkononi mwa Ocean Link lakini Kampuni hii mpya imepata EPZ Exemption mwaka 2012 na je, Serikali haioni kuna harufu ya ufisadi?

Name

Innocent Lugha Bashungwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karagwe

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Jimbo la Siha, lenye sehemu (a),(b) na (c), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upembuzi na utambuzi wa mashamba umekuwa ukifanywa na Serikali kila inapohitajika ili kufanya maamuzi sahihi ya matumizi ya mashamba. Mashamba ya Leoni, Msingi, Pirita na Pongo yanamilikiwa na Vyama vya Ushirika isipokuwa Shamba la Kafoi ambalo linamilikiwa na mtu binafsi. Mashamba haya yalikuwa na migogoro kwa muda mrefu kati ya vyama na wawekezaji ambao kwa sasa migogoro hiyo imekwishatatuliwa. Aidha, Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika inasimamia kwa karibu vyama husika ili kupata wawekezaji wapya kwa maendeleo ya wanachama wa Vyama vya Ushirika na wananchi wa Vijiji vya Wilaya ya Siha.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imechukua hatua kwa viongozi na watendaji waliobainika kujihusisha na ubadhirifu wa mali za KNCU kwa kuwafikisha Mahakamani kwa kesi ya uhujumu uchumi. Aidha, Serikali kwa kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika kutekeleza jukumu lake la ukaguzi wa mara kwa mara kwa Vyama vya Ushirika, itaendelea kufanya ukaguzi kwa Vyama vya Ushirika, ikiwemo KNCU na pale itakapobainika kuwa kuna ubadhirifu wa mali za vyama, Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaohusika bila kujali nyadhifa au uwezo wa aina yoyote walionao.

Mheshimiwa Spika, Shamba la Gararagua limeuzwa na KNCU mwaka 2014 kwa kuzingatia taratibu za manunuzi. Aidha, msamaha wa kodi yaani exemption uliotolewa kwa mwekezaji huyo mwaka 2012 unahusiana na uwekezaji wa Shamba la Kifufu na siyo Gararagua.

Mheshimiwa Spika, kuhusu tuhuma za ufisadi, Wizara itafuatilia suala hilo na itakapobainika kuna viashiria hivyo, Serikali itachukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.