Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 47 2019-02-01

Name

Prof. Norman Adamson Sigalla King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Primary Question

MHE. JORAM I. HONGOLI (K.n.y. MHE. PROF. NORMAN A. S. KING) aliuliza:-

Ili kuboresha utalii katika Hifadhi ya Kitulo, Serikali iliahidi kupeleka wanyama wasio wakali yaani pundamilia 25, lakini mpaka sasa bado wanyama hao hawajapelekwa licha ya Serikali kuahidi kuwa itatekeleza mwezi Mei na Juni mwaka 2018.

(a) Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo?

(b) Je, ni lini Serikali itaongeza aina ya wanyama kama vile paa na swala?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Norman Adamson Sigalla, Mbunge wa Makete, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekwishatekeleza ahadi ya kupeleka Wanyamapori wasio wakali katika hifadhi ya Taifa ya Kitulo mnamo mwezi Oktoba, 2018 ambapo pundamilia 24 walihamishwa katika Hifadhi ya Taifa ya Mikumi na kupelekwa Kitulo. Zaoezi lilifanyika mwezi Oktoba kipindi ambacho hali ya hewa ya Hifadhi ya Taifa ya Kitulo inafanana na hali ya hewa ya Hifadhi ya Taifa ya Mikumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepanga kuongeza pundamilia wengine 26 kutoka Hifadhi ya Taifa ya Mikumi kwenda Hifadhi ya Taifa ya Kitulo, kufikia mwisho wa mwaka 2019/2020. Lengo ni kupandisha idadi ya pundamilia katika Hifadhi ya Kitulo kufikia 50. Pia sambamba na hilo kufikia mwisho wa mwaka wa fedha wa 2019/2020, Serikali inatarajia kupeleka katika Hifadhi ya Taifa ya Kitulo wanyamapori wengine aina ya swala pala wapatao 50 na kuro wapatao 30.