Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 14 2019-01-30

Name

Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Primary Question

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-

Kilwa ni moja kati ya miji mikongwe katika Afrika Mashariki tangu 900 – 1700 AD ikiwemo Lamu, Mombasa, Sofaa na Zanzibar. Miji hii ilipewa heshima ya jina la urithi wa dunia (World Heritage Sights) na husaidiwa na mataifa mbalimbali kama Marekani, Japan, Ujerumani, Uingereza na Taasisi ya UNICEF;

Je, Serikali ya Tanzania inafaidika na nini kutokan kwenye mataifa hayo yanayosaidia nchi zenye Miji ya Urithi wa Dunia?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti,kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya Urithi wa Dunia yanaratibiwa kimataifa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (United Nations Educational, Scientific and Cultural Organization – UNESCO) kupitia mkataba wa mwaka 1972 na ulinzi na uhifadhi wa urithi wa dunia. Mji wa Kilwa una magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara ambayo ni miongoni mwa maeneo ya urithi wa utamaduni ambayo yalipewa hadhi ya urithi wa dunia mwaka 1981. Maeneo mengine ya urithi wa utamaduni yenye hadhi hiyo ni pamoja na Mji Mkongwe wa Zanzibar, Michoro ya mapangoni ya Kolo – Kondoa na urithi mchanganyiko wa Hifadhi ya Bonde la Ngorongoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo manufaa ambayo Serikali ya Tanzania inafaidika kutoka kwa mataifa mbalimbali na nchi wahisani kwa kuwa na maeneo yenye hadhi ya urithi wa dunia. Kuwa na maeneo ya aina hii kunasaidia kuwepo kwa juhudi za pamoja za kimataifa za kuhifadhi, kulinda na kuyaendeleza maeneo haya. Manufaa haya yanaweza kugawanywa katika makundi matatu ambayo ni ushauri wa kiufundi katika masuala ya uhifadhi, misaada ya kifedha na kulitangaza eneo kiutalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya manufaa ambayo Mji wa Kilwa umepata kwa kuwa ni hadhi ya urithi wa dunia ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2002 – 2005 ulifanyika ukarabati wa msikiti mkuu na mdogo pamoja na kubwa, yalitolewa mafunzo kwa mafundi sanifu, ilinunuliwa gari na ukarabati wa boti kwa ufadhili wa Serikali ya Ufaransa wenye thamani ya Euro 660,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2005 - 2008 ulifanyika ukarabati wa Kasri ya Sultani, ununuzi wa mashine ya boti, ukarabati wa nyumba ya wageni ya Kijerumani, ujenzi wa kinga maji eneo la Gereza la Kale na ujenzi wa Birika la Maji la Songo Mnara kwa ufadhili wa UNESCO na Norway wenye thamani ya USD 201,390.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2008 – 2009 yalitolewa mafunzo kwa waongoza wageni, mapishi, usindikaji wa chakula pamoja na uanzishaji wa vikoba kwa wananchi, uandaaji wa kitabu cha urithi wa Kilwa kwa ufadhili wa UNESCO na Serikali ya Ufaransa wenye thamani ya USD 159,780.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2011 – 2014 ukarabati wa majenzi Kilwa Kisiwani na Songo Mnara kwa ufadhili wa Ubalozi wa Marekani wenye thamani ya USD 700,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi hii yote unafanyika kwa kushirikisha wananchi kwa kuwapatia mafunzo ya uhifadhi na kufanya ukarabati wenyewe. Aidha, wananchi wanapatiwa mafunzo ya namna ya kutumia fursa za utalii ikiwa ni pamoja na mafunzo ya uongozaji watalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuishukuru UNESCOna nchi wahisani kwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhifadhi, kuendeleza na kutangaza maeneo haya yenye urithi wa utamaduni.