Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 41 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 346 2018-05-31

Name

Ussi Salum Pondeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chumbuni

Primary Question

MHE. MACHANO OTHMAN SAID (K.n.y. MHE. USSI SALUM PONDEZA AMJADI) aliuliza:-
Vijana wa Kitanzania wanakabiliwa na tatizo sugu la ukosefu wa ajira na hivyo nguvu kazi kupotea badala ya kutumika kwa uzalishaji:-
(a) Je, Jeshi la Kujenga Taifa lina mpango gani wa kutumia nguvu kazi ya vijana kwa kuanzisha miradi ya kilimo cha kisasa ili kuondoa tatizo la ajira?
(b) Je, ni vijana wangapi wamenufaika na ajira kwa kila mwaka kupitia Jeshi la Kujenga Taifa (JKT)?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafunzo ya kijeshi ambayo vijana huyapata kwa muda wa miezi sita, vijana hao pia hujifunza shughuli mbalimbali za uzalishaji mali katika kambi wanazopangiwa baada ya mafunzo ya kijeshi. Shughuli hizo hufanyika ndani ya mwaka mmoja na nusu kati ya miaka miwili ambayo wanajitolea wanapokuwa JKT. Baada ya kumaliza muda huo, tunaamini kwamba vijana wanakuwa wamepata ujuzi ambapo wanaweza kujiajiri au hata kuajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Kujenga Taifa lina mashamba makubwa ya kilimo yanayotumia pembejeo na zana za kisasa za kilimo kama vile mbegu bora, matrekta, mashine za kupandia na mashine za kuvunia (harvesters) hutumika. Mashamba hayo hulimwa kama mashamba darasa kwa ajili ya kuwafundishia vijana walioko JKT. JKT hulima mashamba hayo, si kwa lengo la kuajiri vijana, bali kuwapatia ujuzi ambao watautumia baada ya kumaliza muda wa mafunzo ya JKT. Baada ya kumaliza mafunzo wanaweza kuanzisha miradi ya kilimo cha kisasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafunzo hayo, vijana hupewa mafunzo ya ujasiriamali ikiwa ni pamoja na mafunzo ya ufugaji wa nyama, samaki na nyuki, kupanda na kuvuna miti ya mbao, kuongeza thamani ya mazao ya nafaka na mbegu za mafuta ambayo Wizara ina imani kwamba yatawawezesha vijana hawa kujitegemea kwa kutumia stadi za ufundi, kilimo, mifugo na uvuvi walivyojifunza wakiwa JKT.
Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi ya vijana walioajiriwa na vyombo vya ulinzi na usalama kuanzia mwaka 2003 hadi 2017 jumla yao ni 42,593. Aidha, idadi ya vijana 3,576 wameajiriwa na SUMAJKT Guard Ltd.