Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 41 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 345 2018-05-31

Name

Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-
Viwango vya riba katika benki hapa nchini ni vikubwa na vimekuwa ni kikwazo kwa Watanzania wengi kuweza kukopa na kufanya biashara:-
Je, Serikali inachukua hatua gani ili Benki ziweze kupunguza viwango hivyo vya riba?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara huria ya sekta ya benki ilianza tangu mwaka 1991 mara baada ya kupitishwa wa Sheria ya Usimamizi wa Benki na Vyombo vya Fedha ya mwaka 1991. Kupitia sheria hiyo, wawekezaji walifungua benki binafsi hapa nchini na gharama za huduma za bidhaa kuamuliwa na nguvu ya soko. Hivyo basi kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Benki na Vyombo vya Fedha ya mwaka 1991, Serikali haina mamlaka ya moja kwa moja ya kupunguza viwango vya riba katika soko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ukweli kwamba bei ya huduma na bidhaa katika sekta ya fedha inaamuliwa na nguvu ya soko, Serikali kwa upande wake imekuwa ikichukua hatua za kisera ili kuhakikisha kuwa riba katika soko zinapungua. Baadhi ya hatua zilizochukuliwa na Serikali kupitia Benki Kuu ni kama ifuatavyo:-
(a) Kuzitaka benki za biashara kutumia mfumo wa kuhifadhi na kutoa taarifa za wakopaji (credit reference bureau system).
(b) Kwa sasa Benki Kuu inatoa mikopo ya muda mfupi kwa benki za biashara kwa kiwango cha asilimia 6.89.
(c) Benki Kuu imeshusha riba (discount rate) kutoka asilimia 16.0 hadi asilimia 9.0.
(d) Benki Kuu imepunguza kiwango cha chini cha amana kinachotakiwa kuwekwa Benki Kuu na benki za biashara (Statutory Minimum Reserve Requirement) kutoka asilimia 10.0 hadi asilimia 8.
(e) Serikali imeendelea kulipa malimbikizo ya madai yaliyohakikiwa kwa lengo la kupunguza kiwango cha mikopo chechefu na kuchochea ukuaji wa shughuli za uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hatua hizi za kisera kuchukuliwa na Serikali, baadhi ya benki za biashara hapa nchini zimeanza kupunguza riba ya mikopo. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua za kisera ili kuhakikisha kuwa riba za mikopo katika soko zinaendelea kupungua. (Makofi)