Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 40 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 333 2018-05-30

Name

Selemani Jumanne Zedi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukene

Primary Question

MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza:-
Kata ya Bukene Wilayani Nzega inaundwa kwa Kijiji kimoja tu chenye wakazi zaidi ya 7,600 jambo ambalo linakwamisha uharakishaji wa huduma za maendeleo kwa wananchi. Tulishafuata taratibu zote za kuomba Kijiji cha Bukene kigawanywe ili kupata Kijiji kingine kipya:-
Je, Serikali haioni kuwa siyo sahihi kuwa na Kata inayoundwa na Kijiji kimoja?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Bukene, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, taratibu za kuzingatiwa wakati wa kuanzisha au kupandishwa hadhi maeneo ya utawala zimeelezwa katika Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287 na (Mamlaka za Miji) Sura 288, Toleo la 2002. Sambamba na taratibu hizo upo mwongozo uliofanyiwa marekebisho mwaka 2014 unaofafanua vigezo vya kuzingatiwa katika kuanzisha maeneo hayo ili kuepusha uanzishwaji holela wa maeneo ya utawala yasiyokuwa na sifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo vigezo vinavyopaswa kuzingatiwa katika kuanzisha vijiji. Mapendekezo ya kugawanywa kwa Kijiji cha Bukene kilichopo katika Kata ya Bukene, Halmashauri ya Wilaya ya Nzega hayajawasilishwa rasmi kwa kuzingatia taratibu zilizopo kisheria ikiwa ni pamoja na kujadiliwa na kupitishwa katika vikao vyote vya kisheria ambavyo ni Serikali ya Kijiji, Mkutano Mkuu wa Kijiji, Kamati ya Maendeleo ya Kata, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Kamati ya Ushauri ya Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kipaumbele cha Serikali kwa sasa siyo kuanzisha maeneo mapya ya kiutawala bali kuimarisha maeneo ya kiutawala yaliyopo ili yaweze kutoa huduma stahiki kwa wananchi.