Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 61 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 516 2018-06-29

Name

Alfredina Apolinary Kahigi

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ALFREDINA A. KAHIGI aliuliza:-
Wananchi wa Bukoba Vijijini wanakabiliwa na tatizo kubwa la wanyama waharibifu kama vile ngedere na kadhalika na wanyama hao sasa wanavamia vijiji na kusababisha madhara kwa wananchi:-
Je, Serikali ina mkakati gani madhubuti wa kuwanusuru wananchi wa Bukoba Vijijini na balaa la wanyama hao waharibifu?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Alfredina Apolinary Kahigi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu inatambua uwepo wa tatizo la wanyamapori wakali na waharibifu linalojitokeza katika wilaya zaidi ya 80 hapa nchini ikiwemo Wilaya ya Bukoba Vijijini. Wanyamapori wanaoleta usumbufu kwa wananchi katika wilaya hiyo ni tembo, mamba na ngedere. Tembo kutoka kwenye Ranchi za Kagoma na Mabale wamekuwa wakivamia maeneo ya mashamba na makazi ya wananchi jirani na ranchi hizo. Aidha, mamba wamekuwa wakijeruhi wananchi pembezoni mwa Ziwa Viktoria hususan maeneo ya Kemondo. Vilevile ngedere wanasumbua wananchi kutoka kwenye misitu ya asili ya Kizi, Bugando, Katangarara, Kereuyangereko, Kemondo na Rasina. Misitu hiyo ipo kwenye Kata za Katoma, Karabagaine, Bujogo na Kishongo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imechukua hatua za kudhibiti tatizo hilo kwa kufanya doria ambapo Askari wa Wanyamapori kutoka Kikosi Dhidi ya Ujangili - Mwanza na Pori la Akiba Biharamulo - Burigi - Kimisi (BBK) wakishirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini ambapo waliua jumla ya ngedere 103 na kufukuza makundi kadhaa. Doria hizo zilifanyika katika Kata za kemondo, Katerero, Kanyengereko, Maruku, Katoma, Bujugo, Karabagaine, Nyakato, Kikomela, Ibwela, Nyakibimbili, Kaibanjara, Buterankunzi, Mikoni, Kyamlaile, Lubafu, Kagya, Lukoma, Ruhunga, Buhendangobo na Kishanje. Sambamba na doria hizo, elimu kuhusu mbinu za kujiepusha na kujihami na wanyamapori wakali na waharibifu imetolewa katika kata 21 ka kushirikiana na Maafisa Ugani. Wananchi wameelekezwa mbinu rafiki za kuwafukuza na kuwadhibiti wanyamapori hao wakiwemo ngedere.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu inatambua uhaba wa Askari wa Wanyamapori katika Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini hivyo itaendelea kushirikiana na halmashauri husika katika kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu ili wasilete madhara kwa maisha na mali za wananchi. Hata hivyo, naomba nitoe rai kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini kuajiri Askari wa Wanyamapori kwa ajili ya kuharakisha udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu.