Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 59 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 503 2018-06-27

Name

Maryam Salum Msabaha

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Sekta ya Utalii imekuwa ikitoa ajira kwa vijana wetu wa Visiwani na Tanzania Bara; kutetereka kwa sekta hii kumesababisha kupungua kwa ajira kwa kiasi kikubwa na vijana kurudi mitaani;
Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha na kuboresha sekta hii ili ajira zipatikane kwa wingi?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya utalii ni miongoni mwa sekta muhimu katika uchumi wa Taifa ambapo sekta hii huchangia zaidi ya asilimia 17 ya Pato la Taifa (GDP) na asilimia 25 ya fedha za kigeni nchini. Sekta hii inatoa ajira nyingi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja hapa nchini ambapo kwa sasa sekta ya utalii huchangia ajira takriban 1,500,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango mkubwa wa sekta ya utalii katika kuchangia ajira nchini, Wizara inaendelea na mikakati mbalimbali ya kuongeza fursa za ajira ikihusisha:-
(a) Kupanua wigo wa mazao ya utalii ili kuongeza fursa za ajira kama vile; utalii wa mikutano, utalii wa fukwe, utalii wa matamasha mfano urithi festival, utalii wa miamba (geo-tourism), utalii wa meli, utalii wa reli, mfano TAZARA na Tanga Line, utalii wa michezo, utalii wa matibabu na kadhalika.
(b) Kuhamasisha uwekezaji katika Sekta ya Utalii. Katika kutekeleza hili, Wizara imekamilisha zoezi la kubaini maeneo ya fukwe katika mwambao wa bahari ya Hindi kwa ajili ya uwekezaji wa shughuli za utalii.
(c) Wizara inaendelea kuhamasisha wananchi kuanzisha miradi ya utalii wa utamaduni (Cultural Tourism Programme) ambapo mpaka sasa miradi 66 imeshaanzishwa katika mikoa mbalimbali nchini.
(d) Wizara kupitia Wakala wa Chuo cha Taifa cha Utalii hutoa mafunzo ya kozi za utalii na ukarimu katika ngazi ya astashshada na stashahada. Kozi hizo zimesaidia kupata wahitimu wenye ujuzi unaohitajika katika soko la ajira za sekta ya utalii.
(e) Kuimarisha miundombinu ya usafiri wa anga, nchi kavu na baharini, kuanzisha channel na studio mahsusi kwa ajili ya kutangaza utalii, kuhamasisha wawekezaji kwenye maeneo ya utalii na kuandaa na kutangaza utambulisho wa Taifa (destination branding).
(f) Aidha, Sheria ya Utalii ya mwaka 2008, kifungu cha 58(2), imetenga shughuli mahsusi za biashara ya utalii kwa ajili ya Watanzania. Vile vile, Wizara imepunguza ada ya leseni za biashara ya utalii kwa lengo la kuwawezesha Watanzania wengi kushiriki kufanya shughuli za utalii.