Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 53 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 449 2018-06-19

Name

Dr. Jasmine Tiisekwa Bunga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Vyuo Vikuu

Primary Question

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA aliuliza:-
Mkoa wa Morogoro una vivutio vingi sana vya utalii ambavyo vikitumika vizuri vinaweza kuchangia pato la Taifa na wananchi kwa ujumla; moja kati ya vivutio hivyo ni pamoja na Mbunga za Hifadhi ya Wanyama Mikumi ambayo inaongeza mapato mengi, lakini mbuga hizo hazina hoteli nzuri za kitalii zenye kukidhi viwango vya kimataifa, kutokana na kuungua kwa Hoteli ya Kitalii ya Mikumi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga hoteli kubwa za kitalii ndani ya Mbuga ya Mikumi ili kuvutia watalii wengi?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Jasmine Tisekwa Bunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kuwa Mkoa wa Morogoro una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Hifadhi ya Mikumi. Baada ya kuungua kwa lodge ya Mikumi, Serikali kupitia TANAPA imeendelea na juhudi mbalimbali za kuhamasisha uwekezaji katika hifadhi hiyo, ambao fursa za uwekezaji hususan huduma za malazi zimekuwa zikitangazwa. Aidha, mwekezaji wa kuifufua lodge ya Mikumi alishapatikana na kazi ya ukarabati inaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, watalii wanaotembelea Hifadhi ya Mikumi kwa sasa wanatumia kambi tatu za mahema (tented camps) zilizoko ndani ya hifadhi, lodge na hoteli kumi zilizopo Mikumi Mjini. Wizara kupitia TANAPA imetenga maeneo saba kwa ajili ya uwekezaji wa hoteli na lodge ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Mikumi zenye hadhi na viwango vya kimataifa ili kuleta watalii wengi na kuongeza mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchochea maendeleo ya sekta ya utalii katika Ukanda wa Kusini kwa ujumla, Serikali ilizindua rasmi mradi wa kuendeleza utalii Ukanda wa Kusini wa Tanzania ujulikanao kama REGROW tarehe 12 Februari, 2018 Mjini Iringa. Lengo la mradi huu ni kuwezesha maendeleo ya utalii kwa kuboresha miundombinu, kuhifadhi maliasili na mazingira katika hifadhi ya Ukanda wa Kusini ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Mikumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, napenda kutumia fursa hii kumwomba Mheshimiwa Mbunge, uongozi pamoja na wakazi wa Mikumi kwa ujumla kutenga maeneo ya uwekezaji wa huduma za malazi na utalii ili kunufaika na biashara ya utalii nje ya Hifadhi ya Taifa ya Mikumi. (Makofi)