Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 43 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 364 2018-06-04

Name

Lucia Ursula Michael Mlowe

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Wapo Watumishi katika sekta ya afya, hususan Madaktari na Wauguzi ambao waliajiriwa katika miaka ya 1980 kupitia Serikali Kuu, lakini wakati ule hapakuwa na makato ya mfuko wa kijamii na kuanzia mwaka 1999, Serikali ilianza kuwakata mishahara yao kwenye Mfuko wa PSPF:-
Je, Serikali inawafikiriaje Watumishi hao ambao fedha zao hazikukatwa na mifuko ya kijamii wakati huo hususan Mfuko wa PSPF?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya Julai 1999, mfumo wa malipo ya mafao ya kustaafu kwa watumishi wa Serikali Kuu haukuwa wa kuchangia. Kwa mantiki hiyo, watumishi wote wa umma waliokuwa kwenye ajira ya masharti ya kudumu wanastahili malipo ya uzeeni, wakiwemo watumishi wa sekta ya afya hata kama hawakuchangia. Aidha, kwa mujibu wa Ibara ya tano (5) ya Sheria ya Mfuko wa Pensheni wa PSPF, watumishi wote wa Serikali Kuu ambao waliajiriwa na kuthibitishwa katika ajira ya masharti ya kudumu na pensheni, wanakuwa wanachama wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF kuanzia tarehe ya kuanzishwa kwa mfuko huo.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mafao ya Hitimisho la Kazi Na.2 ya Mwaka 1999 kwa Watumishi wa Umma, ambayo ilianzisha Mfuko wa Pensheni wa PSPF, wastaafu wote ambao ni wanachama wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF na wanaoguswa na Sheria hii wanalipwa mafao yao ya kustaafu na Mfuko wa Pensheni wa PSPF kwa kipindi chote cha utumishi wao. Hii inamaanisha kwamba, mafao yao yanakokotolewa kuanzia tarehe ya kuajiriwa hadi wanapostaafu utumishi wao kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utumishi wa Umma.