Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 43 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 363 2018-06-04

Name

Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Primary Question

MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:-
Mfumo wa ulipaji kodi za kusafirisha bidhaa kutoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara umekuwa ukilalamikiwa kwa muda mrefu kwamba unakwaza na kuvunja harakati za biashara Zanzibar na hivyo kusababisha uchumi wa Zanzibar kushuka:-
Je, Serikali ipo tayari kuunda Kamati kwa ajili ya kushughulikia mfumo wa ulipaji kodi za mizigo kutoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Kombo Hamad, Mbunge wa Wingwi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, chimbuko la malalamiko ya kodi wakati mizigo inaposafirishwa kutoka Zanzibar kuja Tanzania Bara linatokana na kuwepo kwa mifumo tofauti ya kuthamini bidhaa kati ya Zanzibar na Tanzania Bara. Hali hiyo inasababishwa na viwango tofauti vya ushuru wa forodha vinavyopaswa kulipwa kwa bidhaa ya aina moja kutoka nje ya nchi na kusafirishwa kwenda sehemu ya pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Spika, mfumo wa uthaminishaji bidhaa zote zinazoingia Tanzania Bara unafanyika kwa kutumia mifumo ya TANCIS na Import Export Commodity Database ikiratibiwa na kituo cha Huduma za Forodha kilichopo Dar es Salaam. Hata hivyo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitumii mifumo hiyo na hivyo kusababisha kuwepo na tofauti ya kodi kati ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Mheshimiwa Spika, kutokana na utofauti wa mifumo inayotumika, bidhaa zote za nje zinazoingia Tanzania Bara, kupitia Zanzibar hufanyiwa uhakiki licha ya kuwa zimethaminiwa Zanzibar. Iwapo uthamini wa Tanzania Bara utakuwa sawa na ule uliofanywa Zanzibar, hakuna kodi itakayotozwa Tanzania Bara. Ikiwa kodi iliyolipwa Zanzibar ni kidogo, Mamlaka ya Mapato hukusanya tofauti ya kodi iliyozidi.
Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kukusanya tofauti ya kodi kati ya Zanzibar na Tanzania Bara kwa kutumia mifumo ya IECD na TANCIS haina lengo la kuua biashara Zanzibar, hatua hiyo inalenga kuleta usawa wa gharama za kufanya biashara na ushindani hapa nchini.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinaendelea kujadiliana ili kuona kuwa suala hili linapatiwa ufumbuzi wa kudumu. Aidha, kwa kuwa Serikali zetu mbili hazijashindwa kutatua changamoto hii, ni dhahiri kabisa kuwa hakuna sababu ya kuunda Kamati ya kushughulikia mfumo wa ulipaji kodi kwa mizigo inayotoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara. Hata hivyo, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 63(2), Bunge lako Tukufu ni Mhimili unaojitegemea na hivyo Serikali haina mamlaka ya kuunda Kamati ndogo ya Bunge kwa ajili ya jambo hili au jambo lolote lile.