Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 43 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 362 2018-06-04

Name

Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Primary Question

MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU (K.n.y. MHE. MUSSA R. NTIMIZI) aliuliza:-
Barabara ya Buhekela-Miswaki-Loya-Iyumbu inaunganisha Majimbo ya Igunga, Manonga, Igagula na Singida Magharibi, pia inaunganisha Mikoa miwili ya Tabora na Singida, ina Mbuga kubwa ya Wembele ambapo wananchi wanalima mpunga na kulisha Mikoa ya Tabora, Shinyanga na Singida lakini ni mbovu sana:-
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuitengeneza barabara hiyo kwa umuhimu wake huo wa kiuchumi na kimawasiliano?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Buhekela-Miswaki- Loya-Iyumbu inahudumiwa na Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA), katika Halmashauri mbili ambazo ni Halmashauri ya Wilaya ya Igunga yenye kipande chenye urefu wa kilometa 102.79 ambayo ni barabara ya Igunga-Itumba-Simba na Halmashauri ya Wilaya ya Urambo kwa maana ya Uyui yenye kipande chenye urefu wa kilometa 66.05 ambayo ni barabara ya Miswaki - Loya kilometa 28.68 na Loya-Nkongwa kilometa 37.37.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/ 2018, TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Igunga imepanga kufanya matengenezo ya muda maalum kilometa sita na matengenezo ya kawaida kilometa moja kwa gharama ya Sh.225,000,000. Mpaka sasa barabara zenye urefu wa kilometa sita zimeshachongwa na maandalizi ya kuziweka changarawe yanaendelea. Vilevile TARURA Halmashauri ya Igunga imepewa shilingi milioni 297 kwa ajili ya kujenga boksi kalvati tatu na kufanya matengenezo ya muda maalum kilometa 1.6.
Mheshimiwa Spika, mpaka sasa ujenzi wa boksi kalvati tatu umefikia asilimia 30. Katika mwaka wa fedha 2018/2019 TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Igunga imetengewa Sh.165,000,000 kwa ajili ya matengenezo ya sehemu korofi kilometa 23 na ujenzi wa boksi kalvati moja.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Tabora (Uyui) imeidhinishiwa Sh.400,000,000 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya kilometa 20 kwa kiwango cha changarawe pamoja na kujenga kalvati moja. Serikali itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya matengenezo ya barabara hii kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.