Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 42 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 359 2018-06-01

Name

Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Primary Question

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-
Kilwa ni moja ya miji mikongwe katika Afrika Mashariki tangu Anno Domino (AD) 900 -1700 pamoja na miji mingine ya Lamu, Mombasa, Sofala na Zanzibar. Miji hiyo ilipewa heshima ya jina la Urithi wa Dunia (World Heritage Site). Kwa kawaida miji hiyo husaidiwa na Mataifa mbalimbali ikiwemo Marekani, Japan, Ujerumani, Uingereza na Shirika la UNESCO:-
Je, Serikali ya Tanzania imefaidika nini kutoka katika Mataifa hayo yanayosaidia nchi za urithi wa dunia?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohammed Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara yaliorodheshwa kwenye orodha ya Urithi wa Dunia mwaka 1981. Mwaka 2004 eneo la hifadhi la visiwa hivi liliingizwa kwenye orodha ya maeneo yenye urithi ulio hatarini kutoweka (Endangered Site). Hatua hiyo ilisababishwa na hali yake ya uhifadhi kutokidhi kiwango cha Shirika la Umoja wa Mataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni (UNESCO).
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2005, Wizara kwa kushirikiana na UNESCO na nchi za Ufaransa, Norway, Japan na Marekani iliandaa miradi ya kukarabati magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara na mafunzo. Baadhi ya miradi hiyo ni pamoja na mradi wa Euro 600,000 kutoka Serikali ya Ufaransa; Mradi wa Dola za Kimarekani 201,390 kutoka Norway; mradi wa Dola 119,000 kutoka Ufaransa na UNESCO; mradi wa Dola 66,000 kutoka ILO; mradi wa Dola 100,000 kutoka World Monuments Fund; mradi wa Dola 700,000 kutoka Ubalozi wa Marekani; na mradi wa Dola 43,900 kutoka UNESCO. Kukamilika kwa ukarabati kuliwezesha magofu hayo kuondolewa kwenye orodha ya urithi uliokuwa hatarini kutoweka mwaka 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, faida nyingine zilizopatikana ni pamoja na ushauri wa kitalaam na misaada ya vifaa mbalimbali; kuendelezwa kwa miundombinu katika maeneo husika na ongezeko la kipato kwa jamii husika kupitia biashara ya utalii.