Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 50 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 431 2018-06-13

Name

Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Primary Question

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-
Mgogoro wa ardhi katika Hifadhi ya Wanyamapori Selous-Kilwa umechukua nafasi kubwa kati ya Serikali na wananchi wanaoishi karibu na hifadhi hiyo. Mpaka halali haujulikani kwani mwaka 1974 mpaka halali ulikuwa Mto Matandu na mwaka 2010 mpaka huo ulisongezwa mpaka Bwawa la Kilurumila, Kijiji cha Kikulyungu.
Je, Serikali ipo tayari kuhakiki eneo hilo ili kutatua mgogoro uliopo kati yake na wananchi wa Kijiji cha Kihurumile?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Abdallah Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kijiji cha Kikulyungu ni moja ya vijiji tisa vinavyopakana na Pori la Akiba la Selous kwa Wilaya ya Liwale. Ndani ya pori hilo kuna bwawa lijulikanalo kama Kihurumila ambalo ni sehemu muhimu kwa mazalia ya samaki na wanyamapori kama vile mamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miaka1970 wananchi wa Kijiji cha Kikulyungu walikuwa wakivua samaki katika bwawa hilo baada ya kupewa vibali maalum. Hata hivyo, mwaka 1982 Serikali ilizuia shughuli za uvuvi kutokana na baadhi ya wananchi kukiuka taratibu za kuvua samaki ikiwemo matumizi ya sumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka wa Pori la Akiba Selous umewekwa kwa kuzingatia Tangazo la Serikali Na. 275 la mwaka 1974. Tangu wakati huo hadi sasa mpaka huo haujafanyiwa marekebisho yoyote. Hata hivyo, wananchi wa Kijiji cha Kikulyungu hawakubaliani na tafsiri na uhakiki wa mpaka uliofanyika licha ya vijiji vinne kukubaliana na uhakiki huo. Aidha, wananchi wa Kijiji cha Kikulyungu wanadai kwamba Bwawa la Kihurumila ni sehemu ya eneo la kijiji hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ilituma maafisa kuhakiki mipaka ya vijiji vitano kati ya vijiji tisa vinavyounda WMA ya Liwale vinavyopakana na Pori la Akiba la Selous. Vijiji hivyo ni Kimambi, Kikulyungu, Barikiwa, Chimbuko na Ndapata. Uhakiki huo ulishirikisha pia Maafisa kutoka Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi Tanzania, Maafisa Ardhi Wilaya ya Liwale, Taasisi isiyo ya Kiserikali ijulikanayo kama World Wide Fund for Nature (WWF) na wananchi na Viongozi wa Kata na Vijiji vinavyounda Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori ya Liwale. Zoezi hili lililenga kutatua mgogoro wa mpaka na kutangaza WMA ya Liwale. Hata hivyo, wananchi wa Kikulyungu waliwafanyia vurugu watalaam wa Wizara ya Ardhi walipotembelea eneo la mgogoro kwa ajili ya kutafsiri Tangazo la Serikali na kusababisha watalaam kukimbia kuokoa maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia hali hiyo, Wizara imepanga kukutana na viongozi wa Mkoa wa Lindi akiwemo Mheshimiwa Mbunge kwa lengo la kutatua mgogoro huo kwa manufaa ya uhifadhi na ustawi wa wananchi.