Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 44 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 374 2018-06-05

Name

John Wegesa Heche

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. JOHN J. MNYIKA (K.n.y. MHE. JOHN W. HECHE) aliuliza:-
Wilaya ya Tarime ni miongoni mwa Wilaya zinazoongoza kwa wakazi wake kuwa na kesi za kubambikiwa hasa za wizi wa kutumia silaha na mauaji, kitendo kinachokuwa na sura ya kumpa mtuhumiwa wakati mgumu sana kupata msaada wa kisheria.
Je, ni kwa nini Serikali isisaidie upatikanaji wa msaada wa kisheria kwa mahabusu hao ambao kitakwimu ni wengi katika Gereza la Tarime kuliko mashauri mengine yoyote?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ATHONY P. MAVUNDE K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijii kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa utoaji wa msaada wa kisheria kwa watu walioko vizuizini. Kwa kutambua hilo, Sheria ya Msaada wa Kisheria ya mwaka 2017 imetamka wazi kuwa Jeshi la Polisi na Magereza yanapaswa kuweka mazingira ya kuwezesha upatikanaji wa msaada wa kisheria kwa watu walioko vizuizini. Vile vile, kanuni za Sheria hiyo (GN.No. 92018) zimeweka utaratibu wa kufuatwa na Wakuu wa Vituo vya Polisi katika kufanikisha suala hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanikisha upatikanaji wa huduma hii, Wizara imefanya vikao vya mashauriano na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa nyakati tofauti tangu mwaka 2017 kwa lengo la kuweka utaratibu mzuri wa kutekeleza matakwa ya sheria. Hadi kufikia leo tayari rasimu ya mwongozo wa kutoa huduma katika Vituo vya Polisi na Magereza umeandaliwa na utawasilishwa kwa wadau. Pia hivi karibuni Wizara ya Katiba na Sheria itasaini hati ya makubaliano na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa ajili ya kushirikiana katika eneo hili. Jitihada hizi za Serikali zinalenga kuondoa changamoto ya upatikanaji wa msaada wa kisheria katika magereza yote nchini pamoja na gereza la Tarime.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kumwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, pindi Mwongozo huu utakapokamilika yamkini Wilaya ya Tarime inaweza kuwa miongoni mwa wilaya ambazo zitanufaika na huduma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Magereza kwa upande wake yamekuwa na utaratibu wa kutoa huduma ya msaada wa kisheria kwa muda mrefu sasa kwa makubaliano yaliyofanyika kati yao na Shirika la Envirocare ambalo lilikuwa likitoa msaada wa kisheria kwa mahabusu na wafungwa katika baadhi ya mikoa hapa nchini.