Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 20 2018-09-05

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Wananchi wanaoishi katika maeneo yanayopakana na hifadhi za misitu katika Wilaya ya Urambo wamepitia migogoro mingi ya mipaka na hata kuchomewa nyumba na mali:-
Je, ni lini Serikali itamaliza migogoro ya mipaka katika Kata za Nsenda, Uyumbu na Ukondamayo ili wananchi waendelee na kilimo pamoja na shughuli nyingine za kuwaletea maendeleo?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Nsenda na Ukondamoyo ni mojawapo ya kata zinazopakana na Msitu wa Hifadhi wa North Ugalla. Msitu wa Hifadhi wa North Ugalla ulitengwa mwaka 1956 ukiwa na hekta 278,423.3 na kusajiliwa kwa ramani namba 307 chini ya Wilaya ya Tabora. Mwaka 2008 eneo la mpaka wa kaskazini mwa msitu ulipunguzwa kwa zaidi ya umbali wa kilomita tano, sawa na eneo la hekta 114,940.91 kwa ajili ya matumizi ya wananchi. Hivyo, mwaka 2008 eneo la msitu wa North Ugalla lililobaki ni hekta 163,482.39 kwa ramani 2,567 iliyosajiliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu huu umehifadhiwa kwa madhumuni ya kutunza ardhi na udongo eneo la lindimaji (catchment area), kuhifadhi bioanuai, kurekebisha hali ya hewa, kuzalisha mazao ya timbao na yasiyo ya timbao kwa ajili ya kutumiwa kwa utaratibu maalum.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2014, wananchi waliovamia msitu huo waliondolewa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Namba 14 ya mwaka 2002. Hatua zilizochukuliwa za kuondoa migogoro ya mipaka kati ya Vijiji vya Kata za Nsenda na Ukondamoyo ilikuwa; kwanza kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya vijiji husika. Mpango huo uliandaliwa mwaka 2017 na Serikali za Vijiji kwa kushirikiana na Mradi wa Miombo chini ya usimamizi wa Tume ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii ya kutayarisha mpango wa matumizi bora ya ardhi ilifanyika bila ya kuwa mgogoro wowote. Aidha, hati miliki za kimila zinaendelea kutolewa na elimu kuhusu usimamizi shirikishi wa misitu katika vijiji husika. Hatua hii ya utoaji wa elimu kwa wananchi juu ya kutambua, kubaini mipaka halali ya vijiji na mpaka wa hifadhi ya msitu wa North Ugalla zinafanyika kwa ushirikishaji wa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Uyumbu kuna Jumuiya ya Hifadhi ya Jamii ya Wanyamapori ya UWIMA ambayo inaundwa na Vijiji vitatu vya Izimbili, Nsogoro na Izegabatogilwe. Vijiji hivyo vilisaidiwa kutengeneza Mpango wa matumizi bora ya ardhi mwaka 2004. Mwaka 2006 mpaka 2007, baadhi ya wananchi walivamia eneo la ukanda wa malisho linalotumika kama ushoroba. Mwaka 2007 wananchi hao waliondolewa kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kijiji cha Tebhela ambao awali kilikuwa Kitongoji cha kijiji cha Nsogoro walivamia eneo hilo kwa kuweka makazi, kuendesha kilimo na malisho ya mifugo. Hivyo, tatizo lililopo ni uanzishwaji wa eneo jipya la utawala (Kijiji cha Tebhela) bila kuzingatia eneo lililopo. Hata hivyo UWIMA na Halmashauri ya Wilaya ya Urambo wamefanya mikutano kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kuheshimu mipaka ya Hifadhi ya Jamii na matumizi bora ya ardhi.