Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 1 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 14 2018-09-04

Name

Daniel Nicodemus Nsanzugwako

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Primary Question

MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Takwimu za Mpango wa Maendeleo 2016/2017 zimeonesha kuwa Mkoa wa Kigoma ni miongoni mwa Mikoa mitano (5) iliyo maskini zaidi nchini:-
• Je, Serikali inafanya nini kuhakikisha Mikoa hiyo inapata rasilimali fedha na watu ili iweze kuondokana na hali hiyo ya umaskini?
• Je, nini kifanyike kwa Mkoa wa Kigoma ili kujenga ulinganifu katika maendeleo?
• Je, kwa nini Serikali isitenge shilingi bilioni 5 kwa kila mwaka kwa kila Mkoa ili kuondoa kitisho cha Mikoa hiyo kuachwa nyuma kimaendeleo?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel N. Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasuli Mjini, lenye vipengele (a), (b), (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali yetu huzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala, Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na mwaka mmoja mmoja pamoja na Mwongozo wa Bajeti kugawa rasilimali fedha na watu ili kukabiliana na changamoto za umaskini. Aidha, mgawanyo wa rasilimali fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo huenda sambamba na mgawanyo wa rasilimali watu kwa ajili ya utekelezaji, usimamizi, uperembaji na kutoa huduma kulingana na aina ya miradi.
(b) Mheshimiwa Spika, katika kujenga ulinganifu wa maendeleo katika Mkoa wa Kigoma, Serikali imebainisha maeneo na miradi ya kimkakati kwa ajili ya utekelezaji ili kufungua fursa za kiuchumi. Miongoni mwa maeneo ya kimkakati yaliyobainishwa na kuanza kutekelezwa kwenye Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/ 2017 – 2020/2021 ni Mradi wa Upanuzi wa Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma; Mradi wa Uzalishaji wa Umeme wa Maji katika maporomoko ya Mto Malagarasi MW 44.7; kuanzisha na kuendeleza Eneo la Uwekezaji Kigoma (Special Economic Zone); Mradi wa Gridi ya Kaskazini Magharibi KV400; na ujenzi wa Reli ya Kati kwa Kiwango cha Kimataifa.
(c) Mheshimiwa Spika, mgawanyo wa rasilimali fedha huainishwa kwenye Mwongozo wa Bajeti ya Serikali kwa kila mwaka ambao huandaliwa kwa kuzingatia vipaumbele vilivyoainishwa kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano; Dira ya Taifa; na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala. Hoja ya kutenga shilingi bilioni 5 kwa kila Mkoa, kila mwaka ni lazima ifungamanishwe na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala. Hivyo basi, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, kwa sasa Serikali haina Sera wala Mwongozo wa kutenga shilingi bilioni 5 kwa kila mwaka, kwa kila Mkoa ili kukabiliana na changamoto za umaskini.