Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 34 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 289 2018-05-22

Name

Alfredina Apolinary Kahigi

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ALFREDINA A. KAHIGI aliuliza:-
Madarasa na Ofisi za Walimu katika shule mbalimbali katika Mkoa wa Kagera ni mabovu.
Je, Serikali inawasaidiaje wanafunzi wa Kagera kupata mahali pazuri pa kusomea kadhalika na walimu wao wapate ofisi nzuri ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alfredina Apolinary Kahigi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera kuna mahitaji ya vyumba vya madarasa 14,275 kwa shule za msingi, vilivyopo ni 5,934 hivyo upungufu ni 8,341 sawa na asilimia 58. Aidha, mahitaji ya ofisi za walimu ni 1,780, zilizopo ni 925 na upungufu ni 855 sawa na asilimia 48. Kwa upande wa shule za sekondari kuna mahitaji ya vyumba vya madarasa 2,379, vilivyopo ni 1,582 upungufu ni 797 sawa na asilimia 34. Majengo ya Utawala mahitaji ni 212, yaliyopo ni 67 upungufu ni 145 sawa na asilimia 67.
Mheshimiwa Spika, upungufu pia umejitokeza katika miundombinu mingine mfano nyumba za walimu, vyoo na maabara. Hali hii ya upungufu wa miundombinu inatokana na mwamko mkubwa wa wazazi wa kuwaandikisha watoto shule kufuatia Mpango wa Serikali wa Elimu ya Msingi Bila Malipo ambapo idadi ya wanafunzi imeongezeka katika shule za msingi na sekondari.
Mheshimiwa Spika, Serikali itachukua hatua na mikakati mbalimbali za kuhakikisha kuwa wanafunzi na walimu katika Mkoa wa Kagera wanapata mahali pazuri pa kusomea na kufundishia ili kuinua taaluma katika Mkoa wa Kagera. Serikali inaendelea kutoa fedha za ujenzi na ukarabati kupitia mpango wa EP4R ambapo jumla ya shilingi 1,243,600,000 zimetolewa katika Mkoa wa Kagera katika kipindi cha mwaka 2017/2018 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa madarasa, mabweni, maabara, matundu ya vyoo katika shule za Kagemu na Rugambwa zilizoko kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba, Nyailigamba na Profesa Joyce Lazaro Ndalichako katika Halmashauri ya Muleba, Murusagamba katika Halmashauri ya Ngara na Omurwelwe iliyoko Halmashauri ya Karagwe.