Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 33 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 277 2018-05-21

Name

Rashid Mohamed Chuachua

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Masasi Mjini

Primary Question

MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-
Jimbo la Masasi lina shule moja tu ya sekondari kwa kiwango cha Kidato cha Tano na Sita ambayo ni Sekondari ya Wasichana Masasi nayo imekuwa haitoshelezi kutokana na ongezeko la wanafunzi wanaofaulu:-
(a) Je, ni lini Serikali itazipandisha hadhi Shule za Sekondari za Mwenge Mtapika na Anna Abdallah ili ziweze kupokea wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita?
(b) Je, ni lini Serikali itaajiri Walimu katika Jimbo la Masasi ikiwa ikama ya Walimu wa Sayansi katika Shule za Sekondari tisa zilizopo ni Walimu 84 lakini waliopo ni 24 tu?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Mji wa Masasi inazo shule tisa za sekondari. Kati ya hizo, ni shule moja tu ya Masasi wasichana ndiyo ya Kidato cha Tano na Sita. Katika jitihada za kutatua changamoto hiyo, Halmashauri ya Mji wa Masasi imeteua shule mbili za sekondari za Anna Abdallah na Mwenge Mtapika kwa ajili ya upanuzi na kuboresha miundombinu mbalimbali ikiwemo bwalo la chakula, mabweni na jiko ili kuwezesha shule hiyo kuanza kuchukua wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri imewasilisha andiko la mradi wa kukamilisha miundombinu hiyo kwa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwa ajili ya maombi ya fedha za kukamilisha miundominu ya shule hizo. Mara baada ya kukamilika kwa miundombinu hiyo, taratibu nyingine za kuziwezesha shule hizo kuanza kuchukua wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita zitakamilishwa.
• Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutatua changamoto ya Walimu wa Sayansi, Serikali imepeleka Walimu tisa wa masomo ya sayansi katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi mwaka 2017 ili kupunguza uhaba wa Walimu wa Sayansi. Serikali iko kwenye mchakato wa kuajiri Walimu 5,870 wa Shule za Sekondari na watapangwa kwenye maeneo yenye upungufu mkubwa ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Masasi.