Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 29 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 241 2018-05-15

Name

Saul Henry Amon

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rungwe

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI (K.n.y. SAUL H. AMON) aliuliza:-
Jimbo la Rungwe ambalo lina kata 29 lina vituo viwili tu vya afya ambavyo ni Masukulu na Ikati; wananchi wa Kata ya Mpuguso na Isongole kwa nguvu zao wameanzisha ujenzi wa vituo vya afya:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia kumaliza ujenzi huo ili kuwapunguzia adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu katika Hospitali ya Wilaya ambayo baadhi ya maeneo ni takriban kilometa 50 na usafiri usio wa uhakika?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saul Henry Amon, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na uboreshaji wa vituo vya afya 208 nchi nzima ili kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa wagonjwa karibu na wanapoishi. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Serikali imetoa jumla ya shilingi bilioni 1, yaani mwezi Septemba, 2017 ilipeleka Sh.500,000,000 kwenye Kituo cha Afya cha Ikuti kwa ajili ya kujenga jengo la wagonjwa wa nje (OPD), chumba cha upasuaji, wodi ya watoto, wodi ya akina mama wajawazito, jengo la kuhifadhia maiti, jengo la kufulia la kisasa, mtambo wa oxygen na kukarabati miundombinu ili kuhakikisha huduma za upasuaji wa dharura kwa mama wajawazito na huduma nyingine zinapatikana katika Kata ya Ikuti badala ya kufuata huduma hizo kwenye hospitali ya wilaya ambayo iko mbali. Aidha, mwezi Aprili, 2018 Serikali imepeleka Sh.500,000,000 kwenye Kituo cha Afya cha Masukulu ili kujenga na kukarabati miundombinu itakayoboresha huduma kama ilivyo kwa Kituo cha Afya cha Ikuti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, Kituo cha Afya cha Mpuguso kimetengewa shilingi milioni 100 kutoka kwenye mapato ya ndani ya halmashauri kwa ajili ya kumalizia jengo la wagonjwa wa nje (OPD). Sambamba na kuitaka halmashauri itenge fedha za mapato ya ndani ili kuendeleza ujenzi kwenye Kituo cha Afya cha Mpuguso na kuanza ujenzi kwenye Kituo cha Afya cha Isongole, napenda kutoa ahadi kwamba Serikali itavipa vituo hivyo kipaumbele cha juu ili ikiwezekana vikamilike mwakani.