Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 28 Energy and Minerals Wizara ya Madini 240 2018-05-14

Name

Jesca David Kishoa

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA M. MLATA – (K.n.y. MHE. JESCA D. KISHOA) aliuliza:-
Je, Serikali imejipangaje kuwatengea eneo la kuchimba madini katika Mgodi wa Shanta ulioko Mang’onyi (Singida), wachimbaji wadogo wadogo wa Wilaya ya Ikungi na Mkoa wa Singida wanaotegemea kupata kipato kwa shughuli hiyo?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nitoe pole kwa Mheshimiwa Jesca David Kishoa kwa ajali mbaya aliyoipata juzi na kupata maumivu, basi tumwombee kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kupata unafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo, naomba sasa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, nijibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya tarehe 10, Novemba, 2004 na tarehe 1, Aprili, 2005, wachimbaji wadogo wa madini wa Wilaya ya Ikungi waliwasilisha maombi 34 ya leseni ya uchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu katika eneo la Mang’onyi. Hata hivyo, maombi hayo yalikataliwa kutokana na kuombwa juu ya leseni ya utafutaji mkubwa wa madini yenye namba PL 2792/2004 ya Kampuni ya Shanta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kifungu cha 14(1) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017, kinaeleza kuwa mwombaji ambaye maombi yake yalipokelewa kwanza ndiye anayestahili kupewa leseni na hairuhusiwi leseni kutolewa juu ya leseni nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 7(2) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya mamlaka ya utoaji wa leseni, kwa ridhaa ya mmiliki wa leseni, inaweza kutoa leseni zaidi ya moja katika eneo moja la uchimbaji madini iwapo leseni inayoombwa ni ya madini tofauti na leseni iliyopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo mwezi Mei, 2014, Kampuni ya Shanta ilifanya mazungumzo na Kampuni ya Mang’onyi Company Limited ili iachie baadhi ya maeneo ya leseni inayomiliki na kukubali kutoa leseni tatu za uchimbaji wa madini ya dhahabu kwa wachimbaji wadogo wa Vijiji vya Sambaru, Mang’onyi na Mlumbi vilivyopo katika Kata ya Mang’onyi, Wilayani Ikungi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji hivyo vitatu vinazunguka leseni ya Mgodi wa Shanta. Pia kampuni ya Shanta imetoa kwa kikundi cha Aminika Gold Mining Co-operative Society Limited chenye wanachama 193 ambao ni moja ya wanufaika wa leseni hizo, kiasi cha dola za Marekani 25,000 kama fedha za mtaji wa kuendesha shughuli za uchimbani zilitolewa. Aidha, kampuni hiyo imepanga kutoa elimu ya usalama migodini ikifuatiwa na elimu ya uchimbaji ukiwemo uchorongaji wa miamba ili kuwezesha kikundi hicho kufanya shughuli za uchimbaji wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya mazungumzo na kampuni ya uchimbaji wa madini Shanta na kampuni hiyo imekubali kuachia eneo lote la leseni yake ya utafutaji mkubwa wa madini ya dhahabu iliyoko Muhintili Wilaya Ikungi yenye ukubwa takribani kilometa za mraba 71.3 ili itengwe kwa ajili ya uchimbaji mdogo wa madini. Kiasi cha leseni 714 zinatarajiwa kutolea kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa leseni 92 zimekwishatolewa kwa vikundi vya watu binafsi hivyo Wizara inawahimiza wachimbaji wadogo wa madini kuwasilisha maombi yao ili waweze kupatiwa maeneo ya uchimbaji. Hata hivyo, Serikali kupitia Wizara ya Madini itaendelea kutenga maeneo zaidi kwa ajili ya wachimbaji wadogo kwa madini kadri yanavyoweza kupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipekee niishukuru Taifa kubwa Simba Sports Club kwa ushindi walioupata, ahsante sana. (Makofi)