Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 27 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 222 2018-05-11

Name

Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Primary Question

MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya mipaka ya baadhi ya maeneo kama vile mikoa, wilaya na majimbo ya uchaguzi kwani baadhi ya mipaka ya maeneo hayo yana muingiliano unaoleta ugumu wa utoaji wa huduma za jamii?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuligawa Jimbo la Mbinga Vijijini kwa kuzingatia ukubwa wake wa kata 29?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kufanya mapitio ya mipaka kwa baadhi ya mikoa, wilaya na majimbo ya uchaguzi hasa yenye muingiliano unaosababisha ugumu wa utoaji wa huduma za jamii. Hata hivyo, zoezi hilo ambalo linaweza kusababisha mapendekezo ya maeneo mapya ya utawala au kuyahamisha mengine litafanyika baada ya kukamilisha miundombinu ya majengo ya ofisi, majengo ya huduma mbalimbali na vifaa katika mikoa, wilaya na halmashauri mpya zilizoanzishwa tangu mwaka 2012.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imepewa mamlaka ya kuyagawa majimbo ya uchaguzi kwa kuzingatia vigezo vya idadi ya watu, jiografia, hali ya mawasiliano, ukubwa wa jimbo na uwezo wa ukumbi wa Bunge. Ili jimbo ligawanywe Tume hutoa tangazo kuhusu nia hiyo. Baada ya tangazo, mapendekezo hujadiliwa katika vikao vya halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa na hatimaye huwasilishwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo hutangaza Jimbo jipya baada ya kupata kibali cha Rais.