Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 17 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 138 2018-04-25

Name

Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA aliuliza:-
Kiwango cha elimu katika Mkoa wa Tabora kimeshuka sana, Mkoa umefanya vibaya katika mtihani wa darasa la saba, kidato cha nne na cha sita. Kufanya vibaya kunatokana na changamoto mbalimbali kama walimu, upungufu wa madawati na idadi kubwa ya wanafunzi katika madarasa.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kero hizi zinatatuliwa ili kurejesha hadhi ya elimu Mkoa wa Tabora?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, ambaye ni mtoto wa shangazi yangu na Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto zilizotajwa katika swali, si kweli kwamba kiwango cha elimu kimeshuka sana Mkoani Tabora kwa kufanya vibaya kwenye mitihani. Takwimu zinathibitisha hali tofauti kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, katika mitihani ya darasa la saba ya mwaa 2016 kiwango cha ufaulu kilikuwa asilimia 71.35 ambapo Mkoa wa Tabora ulishika nafasi ya 10 kitaifa, lakini mwaka 2017 ufaulu ulipanda hadi asilimia 73.61 na Mkoa ukaendelea kushika nafasi ya 10 kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, katika mitihani ya kidato cha nne ya mwaka 2016 kiwango cha ufaulu kilikuwa asilimia 71 ambapo Mkoa wa Tabora ulishika nafasi ya 10 kitaifa, lakini mwaka 2017 ufaulu ulipanda hadi asilimia 84 na Mkoa kushika nafasi ya 3 Kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kwa upande wa kidato cha sita, ufaulu mwaka 2016 ulikuwa asilimia 97.8 na Mkoa wa Tabora ulishika nafasi ya 11 kitaifa. Kwa mwaka 2017 pamoja na takwimu kuonesha kuwa ufaulu ulikuwa asilimia 87, nafasi ya mkoa kitaifa ilipanda hadi nafasi ya 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka yote miwili mfululizo, Mkoa wa Tabora umekuwa juu ya wastani wa ufaulu kitaifa, hilo ni jambo la kujivunia. Kwa hali hiyo hatuwezei kusema kiwango cha elimu katika Mkoa wa Tabora kimeshuka bali kimepanda. Serikali ina kila sababu ya kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mheshimiwa Aggrey Mwanri na viongozi wote wa Mkoa wa Tabora wakiwemo viongozi wa wilaya zote na hamashauri zote kwa juhudi zao zilizowezesha matokeo hayo mazuri.