Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 15 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 119 2018-04-23

Name

Jamal Kassim Ali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Magomeni

Primary Question

MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. JAMAL KASSIM ALI) aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kulifanyia Shirika la Umeme (TANESCO) lijiendeshe kwa faida?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jamal Kassim Ali, Mbunge wa Magomeni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) linakabiliwa na gharama kubwa za uendeshaji ambapo zaidi ya asilimia 80 ya gharama zinatokana na uzalishaji wa umeme, ukarabati wa mitambo na miundombinu mingine muhimu ya umeme. Mapato ya Shirika yamekuwa hayakidhi vya kutosha gharama za uendeshaji hususan katika maeneo ya uzalishaji wa umeme kwa kutumia mafuta mazito ambayo ni ghali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika pia linakabiliwa na tatizo la malimbizo ya madeni ya wateja wakubwa, wa kawaida na wadogo kushindwa kulipa ankara za umeme kwa wakati zikiwemo Taasisi na Mashirika ya Umma pamoja na wateja wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mikakati madhubuti ya kuliwezesha Shirika la TANESCO kujiendesha kibiashara na kuondokana na hasara. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kufanya uwekezaji katika mitambo ya kufua umeme kwa kutumia gesi asilia na maji ili kuepukana na mitambo inayotumia mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari mipango inaendelea kuanza utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa megawati 2100 wa Rufiji Stigler’s Gorge utakaozalisha umeme kwa gharama nafuu na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za kuzalisha umeme na kulifanya Shirika lijiendeshe kibiashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingine ni megawati 300 zitokanazo na gesi asilia eneo la Mtwara pamoja na megawati 330 katika eneo la Somangafungu Mkoani Lindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha karibuni, maeneo ya Kibiti, Ikwiriri na Ngara yameunganishwa katika gridi ya Taifa, hivyo kupelekea kupunguza gharama za uendeshaji iliyokuwa ikitokana na matumizi ya mafuta mazito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango mingine ya Serikali ni kuunganisha baadhi ya maeneo katika Gridi ya Taifa kwa utekelezaji wa miradi ya njia kusafirisha umeme kwa Mikoa ya Ruvuma, Rukwa na Kigoma na hivyo kuachana na mitambo inayozalisha umeme kwa mafuta ambayo ni ghali. Ahsante sana.